Serikali imesema imeanza kuchukua hatua mbalimbali kubaini chanzo cha tabia ya baadhi ya wanafunzi kuandika lugha zisizostahili kwenye karatasi za mitihani ya kitaifa, ikieleza kuwa tatizo hilo linachangiwa na sababu za kijamii, kisaikolojia na kimazingira.
Kauli hiyo imetolewa bungeni na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Mhe. Wanu Ameir, alipokuwa akijibu swali la Mbunge aliyehoji hatua zinazochukuliwa na serikali kubaini chanzo cha wanafunzi kutumia lugha zisizofaa kwenye mitihani.
Waziri amesema kuwa mwaka 2025, Serikali kupitia Baraza la Mitihani Tanzania (NECTA) ilifanya utafiti uliobaini kuwa sababu za tabia hiyo ni pamoja na mmomonyoko wa maadili, msongo wa mawazo, kukata tamaa pamoja na mazingira yanayowazunguka wanafunzi.
Ameongeza kuwa kwa mujibu wa kanuni za NECTA, mwanafunzi anayebainika kuandika lugha zisizostahili kwenye karatasi ya mtihani hukumbana na adhabu ya kufutiwa matokeo ya mtihani husika.
Aidha, Serikali imekuwa ikizifuatilia shule zinazobainika kuwa na matukio ya aina hiyo ili kubaini iwapo kuna ushawishi wowote unaotolewa kwa wanafunzi hao.
Katika hatua nyingine, Waziri amesema Serikali inaendelea kutoa elimu ya maadili kwa jamii, kuimarisha huduma za ushauri nasaha shuleni, pamoja na kuendesha kampeni za kuwajengea wazazi uelewa kuhusu malezi bora ili kupunguza changamoto za kisaikolojia kwa wanafunzi.
Akijibu swali la nyongeza, Waziri amesema Serikali imeunda kikosi kazi maalum cha kitaifa kuchunguza kwa kina chanzo cha tabia hiyo, ikiwemo madai ya baadhi ya wazazi kuwashawishi watoto wao kuandika lugha zisizostahili ili kufutiwa matokeo ya mitihani.
Amesema baada ya uchunguzi kukamilika, taarifa itawasilishwa serikalini na hatua stahiki zitachukuliwa kwa mujibu wa sheria na taratibu zilizopo.





