Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Ashatu Kijaji, amesema Tanzania inatarajia kunufaika kwa kiasi kikubwa kiuchumi kupitia utalii wa mikutano na matukio (MICE), unaochangia ongezeko la watalii, ajira na Pato la Taifa.
Akizungumza Bungeni leo Mei 15, 2026 wakati akiwasilisha Bajeti ya Wizara hiyo, Dkt. Kijaji ametaja matukio manne makubwa ya kimataifa yatakayofanyika nchini ambayo yanaweza kuleta fursa mpya kwa sekta ya utalii.
Miongoni mwa matukio hayo ni Mkutano wa 153 wa Umoja wa Mabunge Duniani (IPU) unaotarajiwa kufanyika Arusha Oktoba 5–9, 2026 na kuhudhuriwa na zaidi ya washiriki 1,500 wakiwemo Maspika 183. Amesema Wizara itaandaa vifurushi vya utalii vitakavyowezesha wageni kufanya booking moja kwa moja kupitia tovuti ya IPU, pamoja na kuweka mabanda ya utalii katika eneo la mkutano.
Dkt. Kijaji pia ametaja tukio la World Travel Awards (WTA) litakalofanyika Desemba 2026 nchini, likitarajiwa kuhudhuriwa na zaidi ya washiriki 1,000 kutoka mabara mbalimbali. Amesema Wizara itatumia majukwaa ya kidijitali, machapisho na booking platform ya TTB kutangaza vivutio vya Tanzania.
Tukio la tatu ni Mashindano ya Miss World 2027, yatakayofanyika Mei 2027 nchini, yakitarajiwa kuvutia takribani watu 20,000 wakiwemo washindani 120. Wizara imeeleza itatumia vyombo vya habari vya ndani na nje pamoja na kuandaa ziara maalumu (FAM Trip) kwa washiriki na waandishi wa habari ili kutangaza vivutio vya Tanzania.
Aidha, Waziri ametaja Fainali za AFCON 2027 zitakazoandaliwa kwa pamoja na Tanzania pamoja na nchi nyingine za Afrika Mashariki. Amesema mashindano hayo yanatarajiwa kufuatiliwa na watazamaji wa viwanjani milioni 1.8 na zaidi ya bilioni 1.9 kupitia televisheni duniani, huku yakikadiriwa kuingiza faida ya zaidi ya Dola za Marekani bilioni 2.
Kwa mujibu wa Dkt. Kijaji, Wizara itaendelea kuboresha miundombinu ikiwemo barabara, viwanja vya ndege na malazi katika maeneo ya utalii, pamoja na kuimarisha huduma kwa kuwanoa watoa huduma za utalii. Amesema pia vifurushi maalum vitaandaliwa kwa ajili ya wageni wa AFCON na kampeni za utangazaji zitaendelea hata baada ya mashindano kumalizika.





