MILAN, Italia
MSIMU uliopita haukuwa mzuri kwa Inter Milan baada ya kuambulia patupu katika mashindano yote matatu ya ndani. Safari hii, upepo umebadilika.
Inter wametwaa ubingwa wa Ligi Kuu (Serie A) walipoifunga Lazio mabao 2-0, ushindi uliowaweka kileleni kwa tofauti ya pointi 12 dhidi ya Napoli inayoshika nafasi ya pili.
Zikiwa zimebaki mechi tatu kwa kila timu, si Napoli wala timu yoyote ya Serie A inayoweza kufikia pointi hizo.
Timu hiyo sasa inasubiri fainali ya Kombe la Ligi, ambapo itaikabili Lazio, mchezo ukitarajiwa kuchezwa Mei 13, 2026.
Endapo Inter itashinda, basi itakuwa imemaliza msimu ikiwa na mataji makubwa mawili ya ndani, jambo ambalo halijawahi kutokea tangu mwaka 2010 ikiwa chini ya kocha Jose Mourinho.
Msimu uliopita, Inter walikuwa na nafasi ya kutwaa mataji matatu (Serie A, Kombe la Ligi na Ligi ya Mabingwa) lakini yote yaliota mbawa.
Walilikosa taji la Serie A kwa tofauti ya pointi moja nyuma ya Napoli iliyotwaa ubingwa, waliishia nusu fainali ya Kombe la Ligi, na pia walipoteza fainali ya Ligi ya Mabingwa kwa kufungwa mabao 5-0 na PSG.
Katika mazingira yaliyowashitua wengi, kocha Simone Inzaghi, ambaye aliifikisha mara mbili fainali ya Ligi ya Mabingwa, alijizulu na kutimkia Al-Hilal ya Saudi Arabia.
Licha ya wengi kuponda uamuzi wa Inter kumpa ajira Cristian Chivu kwa madai ya uzoefu wake mdogo, akiiongoza Parma katika mechi 13 pekee za Serie A, ni wazi beki huyo wa zamani amewajibu kwa vitendo.
Kwa upande wao, mabingwa watetezi, Napoli, hawakuwa na upepo mzuri kwani mshambuliaji wao tegemeo, Romelu Lukaku, aliumia kabla ya msimu kuanza na kukosekana kwa miezi kadhaa.
Ni kama ilivyokuwa kwa Kevin De Bruyne, Frank Anguissa, David Neres, Billy Gilmour na Amir Rrahmani, ambao pia walikosa mechi nyingi kutokana na majeraha.
Imeandaliwa na Hassan Mwasha






