MANCHESTER, Uingereza
BAADA ya ushindi wa mabao 3-2 dhidi ya Liverpool jana Mei 3, 2026, Manchester United imefuzu kushiriki michuano ya Shirikisho la Soka la Ulaya (UEFA) ya Ligi ya Mabingwa msimu ujao.
Katika mchezo huo, nahodha Bruno Fernandes alihusika katika bao la ushindi la Kobie Mainoo, hivyo kuandika historia klabuni hapo.
Bruno anakuwa mchezaji pekee wa Man United aliyetengeneza nafasi nyingi (120) msimu huu, akivunja rekodi iliyodumu klabuni hapo tangu msimu wa 2003-04.
Mtanange huo uliishuhudia Man United ikipata mabao yake kupitia kwa Benjamin Sesko, Matheus Cunha na Mainoo.
Kwa sasa, Bruno amebakiza asisti moja kuifikia rekodi ya Thierry Henry na Kevin De Bruyne, ambao ndiyo wachezaji pekee kufikisha 20 ndani ya msimu mmoja wa Ligi.
Baada ya kujihakikishia nafasi ya kucheza Ligi ya Mabingwa msimu ujao, Man United itarejea dimbani Mei 9, 2026 kuikabili Sunderland, kabla ya kucheza na Nottingham Forest.






