LONDON, Uingereza
KIUNGO wa zamani wa Chelsea, Emmanuel Petit, ameishauri klabu hiyo kumsajili mpachikaji mabao wa Galatasaray raia wa Nigeria, Victor Osimhen.
Chelsea imekuwa haina bahati katika usajili wa straika tangu Didier Drogba alipoondoka klabuni hapo miaka mingi iliyopita.
Hata hivyo, Petit anaamini Osimhen atamaliza mkosi uliowakumba washambuliaji wa kati wengi waliojaribu kuvaa viatu vya Drogba.
“Tangu Drogba alipoondoka, nafikiri jezi namba 9 ya Chelsea imekuwa na mkosi. Nafikiri itakuwa tofauti kwa Osimhen …” amesema Petit.
Hata hivyo, Osimhen anayesakwa pia na klabu za Barcelona, Real Madrid, Bayern Munich na PSG, amesema anatamani kubaki Galatasaray kwa miaka mingi ijayo.






