CATALUNYA, Hispania
KOCHA wa zamani wa Barcelona, Xavi, amefichua kuwa alikaribia kumrejesha Lionel Messi lakini Rais wa klabu hiyo, Joan Laporta, alikataa mpango huo.
Xavi anazungumzia mwaka 2023, ambapo akiwa kocha wa klabu hiyo aliiwezesha kutwaa mataji mawili kwa mpigo.
Katika mahojiano yake ya hivi karibuni, Mhispania huyo amesema si Messi pekee, bali pia alijaribu kuwarudisha Neymar na Pedro.
“Nikiwa kocha wa Barcelona, nilimrejesha Dani Alves na nilijaribu kufanya hivyo pia kwa Neymar, Pedro na Messi.
“Pedro na Neymar ilishindikana kutokana na hali ngumu ya kiuchumi lakini kwa Messi ni Rais ndiye aliyekataa,” amesema.
Kwa mujibu wake, yalikuwepo mazungumzo yaliyochukua miezi mitano kati yake na Messi. “Kila kitu kilikuwa kinaenda vizuri, lakini mwisho wa siku Rais alikataa.”






