Urusi imevuta hisia za dunia baada ya kuandaa sherehe ya mfano ya harusi kati ya roboti wawili wenye umbo la binadamu (humanoid robots), tukio lililofanyika jijini Moscow katika Maktaba ya Pushkin. Roboti hao wanaojulikana kama Robert na Matilda walitangazwa kuwa “wanandoa wa roboti” mbele ya wageni waliohudhuria, huku wakibadilishana viapo vya mfano na vikuku vya harusi.
Katika hafla hiyo, kila roboti alipewa tabia maalumu; Robert ameundwa kuigiza mfanyakazi wa ofisini na mwanablogu, huku Matilda akiwa na muonekano unaofanana na mcheza ballet. Kwa mujibu wa taarifa, roboti hao walitambulishwa awali katika Kongamano la Kimataifa la Uchumi la St. Petersburg (SPIEF 2026), kabla ya kushiriki tukio hilo lililolenga kuonyesha maendeleo ya teknolojia ya Akili Bandia (AI).
Ingawa harusi hiyo haikuwa ya kisheria bali ilikuwa ya mfano, imeibua mjadala kuhusu nafasi ya roboti wenye akili bandia katika maisha ya binadamu siku zijazo. Wataalamu wanaeleza kuwa matukio kama haya yanaonyesha kasi ya maendeleo ya teknolojia, huku yakichochea mjadala kuhusu uhusiano unaoweza kujengwa kati ya binadamu na mashine.
