Thursday, June 26, 2025
spot_img

POLISI ANAYETESA WAKULIMA KIJIJI CHA IYALA MUONGO

Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Mbeya (RPC) Irlich Matei

 

MWANDISHI WA PANORAMA

ASKARI Polisi Endeni Mgonja wa Kituo cha Polisi Chimara, Mbeya, ambaye ushahidi wa nyaraka na mahojiano umethibitisha pasipo shaka kuwa amekuwa akifanya vitendo vya kikatili dhidi ya wakulima wa Kijiji cha Iyala kilichopo Wilaya ya Mbarali, ni muongo.

Polisi Endeni ambaye ametuhumiwa na wakulima hao kupora kwa mabavu mradi wa ujenzi wa banio la maji katika mashamba ya wanakijiji, kuwalazimisha wamlipe debe sita za mpunga katika kila ekari moja wanayovuna na kuwaweka korokoroni wanaokataa kutii amri yake, alikanusha madai yote katika mahojiano yake ya awali na Tanzania PANORAMA.

Hata hivyo, ushahidi wa nyaraka na ule wa mahojiano baina Tanzania PANORAMA na baadhi ya wakulima hao, umethibitisha pasipo chembe ya shaka kuwa Polisi Mgonja amepora mradi huo kwa mabavu, anawadai wakulima wa Iyala wamlipe debe sita za mpunga katika kila ekari moja wanayovuna na anawaweka mahabusu wanaokataa kutii amri ya kumpa mazao anayoyataka.

Polisi Endeni katika mahojiano ya awali kuhusu tuhuma anazoelekezewa alikanusha kwa sauti thabiti kuwa hahusiki nazo kwa namna yoyote ile na kwamba hajawahi kufika kwenye mashamba ya wakulima wa Iyala, hafanyi biashara ya aina yoyote na hamfahamu wala hamdai chochote aliyesaini mkataba wa ujenzi wa banio hilo, Atanasi Yusuph Yawanga.

Kwa maneno yake mwenyewe alisema, “Hayo mambo siyajui kabisa kabisa. Tangu nizaliwe na kuja hapa Chimara sijawahi kufika kwenye mashamba ya wanakijiji hao, mimi sifanyi biashara yoyote, ni askari tu na huyo Atanasi Yusuph Yawanga ndiyo kwanza namsikia kwako, simfahamu kabisa mtu wa aina hiyo.

Aidha, Polisi Mgonja alikanusha tuhuma za kuwaweka wakulima mahabusu akiwashinikiza wamlipe debe sita za mpunga kwa kila ekari moja wanayovuna kama malipo anayostahili kwa ujenzi wa banio.

Alisema “Kama sijafika kwenye hayo mashamba nawawekaje ndani sasa. Na kwanini unaniuliza hayo maswali, kwani hata kama ni kweli si utaandika, haya itasomwa, ndiyo kitabadilika nini?” alihoji.

Muda mfupi baada ya mahojiano hayo, polisi huyo alituma pesa kidogo kwa Tanzania PANORAMA, akitumia laini tofauti na aliyopigiwa na alipoulizwa fedha hizo ni za kazi gani alisema alikuwa anajaribu kutuma.

Tofauti kabisa na kanusho hilo la Polisi Mgonja, nyaraka ambazo Tanzania PANORAMA imeziona zinaonyesha kuwa ana mgogoro wa muda mrefu na wakulima ambao walipata kumuomba mkuu wa kituo chake cha kazi, (Mkuu wa Kituo cha Polisi Chimara OCS), Antipas Temu amchukulie hatua, jambo ambalo hakulitekeleza.


Moja ya nyaraka ambazo Tanzania PANORAMA imeziona zinazomuhusisha moja kwa moja Polisi Mgonja na tuhuma anazodaiwa kuwafanyia wakulima wa Iyala, iliyoandikwa na Afisa Mtendaji wa Kijiji cha Iyala kwenda Kituo cha Polisi Chimara inaomba kukamatwa kwa Polisi Mgonja na familia ya Atanasi Yawanga kwa kukaidi amri ya mtendaji huyo.

Barua hiyo ya Septemba 4, 2020, iliyosainiwa na kugongwa muhuri na Afisa Mtendaji wa Kijiji cha Iyala, inaeleza kuwa Septemba 3, 2020 kilifanyika kikao kilichowahusisha mtendaji huyo, Polisi Mgonja, familia ya Yawanga na Halmashauri ya Kijiji, kikao ambacho ajenda yake kuu ilikuwa kutatua mgogoro wa ujenzi wa banio la maji kati ya wabia wawili wa ujenzi wa mradi huo ambao ni Yawanga na John Jonathan Shillinde.

Barua hiyo inaeleza, iliafikiwa na pande zote katika kikao hicho kuwa kazi zote za ujenzi wa banio la maji zisitishwe hadi Septemba 7, 2020 ambapo uamuzi wa mgogoro huo utatolewa lakini Polisi Mgonja na familia ya Yawanga walipuuza wakaendelea na ujenzi.

Aidha, mkataba wa ujenzi wa banio hilo ambao Tanzania PANORAMA imeuona unaonyesha kusainiwa Mei, 2019 na watu wawili, Atanasi Yusuph Yawanga wa Chimara, Mbarali na John Jonathan Shillinde wa Mbeya.

Mkataba huo unamtaja Yawanga kama mshiriki namba moja aliyekosa nguvu ya kutekeleza mradi wa ujenzi wa banio la maji kwenye mashamba mapya ya Kijiji cha Iyala aliopewa na kijiji hicho na kwamba, alimuomba Shillinde anayetajwa kama mshiriki namba mbili washirikiane kuutekeleza.

Pamoja na mambo mengine katika mkataba huo, sharti namba tano linasomeka, ‘ kwamba gharama za utengenezaji wa miundombinu husika zimekubalika kugharimu kiasi cha shilingi milioni mia moja na ishirini (120,000,000) na endepo zitazidi kiasi tajwa kwenye aya hii basi wahusika watalazimika kwenda kwa mwanasheria kutambua mabadiliko hayo.’

Na aya ya nne inasomeka, ‘kwamba imekubalika mshikiri namba 1 ametimiza jukumu lake la kupata kazi ya utengenezaji wa miundombinu kwenye mashamba mapya ya Kijiji cha Iyala na imekubalika na wahusika wa mkataba kuwa gharama ambazo mshiriki namba 1 ametumia ni Shilingi Milioni Hamsini na Tatu na Laki Sita (53, 600,000) tu.’

Taarifa zaidi zinaonyesha kuwa mbali ya Shilingi milioni 53,6000 zilizotumiwa na Yawanga kupata zabuni ya mradi huo, gharama nyingine zote za ujenzi wa miundombinu zilibebwa na Shillinde ambaye hata hivyo alivurumushwa baada ya Yawanga kuanza kukiuka masharti ya mkataba kabla ya kumkaribisha Polisi Mgonja kwenye utekelezaji wa mradi.

Shamba la mpunga Mbarali



Mmoja wa wanakijiji waliozungumza na Tanzania PANORAMA ameeleza kuwa Shillinde baada ya kutupiwa virago huku akidhulumiwa pesa zake zote alizotumia katika ujenzi wa banio alikwenda kulalamika kwa OCS Temu lakini aliambulia kutishwa na mkuu huyo wa kituo kabla ya kutimuliwa.

Aidha, anaeleza zaidi kuwa, Polisi Mgonja amekuwa akiwaweka mahabusu bila kuwafungulia mashtaka wakulima wanaokataa kumpatia mazao yao kama alivyoagiza na anawataja wajumbe watatu wa kijiji kuwa watu waliotiwa ndani hivi karibuni.  

Alipotafutwa na kuulizwa kuhusu sakata hilo, Mkuu wa Kituo cha Polisi Chimara, Temu alisema mwenye mamlaka ya kuzungumza kwa niaba ya Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya ni Kamanda wa Polisi wa Mkoa (RPC) Irlich Matei.

Polisi Mgonja alipotafutwa na kuulizwa ni kwa nini amesema uongo kuwa hahusiki katika mgogoro wa ujenzi wa banio hilo, hahusiki kuwatia ndani wakulima wanaokataa kumlipa mazao yao na hamfahamu mzabuni wa kandarasi hiyo huku akijua kuna nyaraka zinazomuhusisha na matendo yote hayo, alikata simu na alipopigiwa tena na tena hakupokea.

Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Mbeya, RPC Matei jana hakupatikana kuzungumzia mambo mapya yaliyoibuka katika mgogoro huo.

Nyingine Zinazohusiana na Hii

1 COMMENT

  1. Mbona kichwa Cha hbar hakiendani na story by the way washaur wananchi waende mahakaman hiki mnachofanya ni kuchafuana

Leave a Reply to Anonymous Cancel reply

Please enter your comment!
Please enter your name here

Tufuatilie

0FansLike
3,913FollowersFollow
0SubscribersSubscribe
- Advertisement -spot_img

Habari Nyingine Mpya