![]() |
Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Mbeya (RPC), Urlich Matei |
MWANDISHI WA PANORAMA
ASKARI Polisi, Endeni Mgonja wa Kituo cha Polisi Chimara, Mbeya, anadaiwa kupora kwa mabavu mradi wa ujenzi wa banio la maji katika mashamba ya wakulima wa Kijiji cha Iyala, Wilaya ya Mbarali, Mkoa wa Mbeya.
Sambamba na uporaji huo, Polisi Mgonja anadaiwa, kwa kutumia upolisi wake amekuwa akiwaweka korokoroni wanakijiji wanaokataa kumlipa madebe sita ya mpunga kwa kila ekari moja wanayovuna kama gharama zake za ujenzi wa banio hilo, akishinikiza wakubali kumlipa ndipo awaachie huru.
Madai haya yametolewa na wakulima wa Kijiji cha Iyala katika mahojiano yao na Tanzania PANORAMA Blog kuhusu kile walichodai kuwa ni unyanyasaji unaofanywa na polisi huyo akishirikiana na wenzake pamoja na kuishi maisha ya wasiwasi kutokana na kutishiwa kufunguliwa kesi na kutiwa korokoroni pasipo kutenda makosa.
Huku wakionyesha nyaraka zinazohusiana na mgogoro wa mradi wa ujenzi wa banio hilo pamoja na kulazimishwa kumlipa polisi Mgonja madebe sita ya mpunga kwa kila ekari moja wanayovuma, walidai hakuna makubaliano waliyoingia naye kumlipa mavuno yao bali anawalazimisha kutekeleza hilo kufidia deni analomdai mkandarasi wa mradi huo ambaye Tanzania PANORAMA imeona mkataba wake wa ubia alioingia kujenga banio hilo.
Mmoja wa wanakijiji hao, jina lake tumelihifadhi kwa sababu ya usalama wake kutokana na madai aliyoyatoa kuwa maisha yake yatakuwa hatarini iwapo atabainika ameongea na waandishi wa habari, alisema mjenzi wa banio hilo anayetambulika na wanakijiji ni Atanasi Yusuph Yawanga, mkazi wa Chimara, Wilaya ya Mbarali, Mkoa wa Mbeya.
![]() |
Shamba la mpunga lililoko Mbarali |
“Huyu polisi ni mnyama, anatunyanyasa sana, anatukamata wanakijiji akitulazimisha tumlipe madebe sita ya mpunga kwa kila ekari moja tunayovuna kama malipo ya ujenzi wa banio la maji katika mashaba yetu wakati sisi hatumtambui, tunayemtambua ni Atanasi Yusuph Yawanga na mwenzake John Jonathan Shillinde, ndiyo wana mkataba wa ujenzi wa banio hilo.
“Sasa tunasikia Yawanga anadaiwa na huyo polisi na hakuwa na fedha za kumlipa, kwa hiyo aliamua kumshughulikia mjenzi mwenzie huyo Shillinde na yeye hatujui alikofia kwa sababu polisi walimuandama kweli, akaondolewa kwenye ujenzi na akadhulumiwa fedha zake zote alizotumia kwenye ujenzi huo ndipo akaingizwa huyu polisi kwa makubaliano yao wenyewe kuwa tutalipa sisi mavuno yetu lakini bila sisi kutushirikisha.
“Hilo jambo tunaliona ni unyama kabisa, kuchukua mazao yetu kwa nguvu, tukipinga ndiyo tunaanza kukamatwa, wengine wana kesi, wengine wanawekwa ndani wanalazimishwa wakubali kumpa mpunga anaotaka na wakikubali ndiyo wanaachiwa ni unyama. Kabla hatujaja kuzungumza na nyinyi tumeacha wenzetu watatu waliokataa kumpa mpunga Polisi Mgonja wako ndani.
“Tumelalamika sana kuhusu huu unyama kwa sababu huku ni kutunyang’anya mazao yetu kwa nguvu, tulienda kwa mkuu wa kituo lakini naye ndiyo akawa anaruhusu tuwekwe ndani bila makosa, tumekwenda mpaka kwa Kamanda wa Polisi wa Mkoa lakini hakuna msaada tuliopata, tunazidi kuteswa tu na kunyang’anywa mazao yetu. Sasa kwa sababu wakubwa zaidi hatuwezi kuwafikia maana hatutapa ruhusa kuwaona na waandishi wa kule hakuna wa kuandika, ndiyo tukaona tuje tusemee huku wakubwa wasikie waje watuokoe na mateso na unyama wa huyu polisi Mgonja,” alisema.
Alipoulizwa polisi Mgonja kuhusu tuhuma hizo alikanusha na kueleza kuwa hahusiki nazo kwa namna yoyote ile na kwamba hajawahi kufika kwenye mashamba ya wanakijiji hao, hafanyi biashara ya aina yoyote, hamfahamu Atanasi Yusuph Yawanga na wala hamdai kiasi chochote cha fedha.
“Hayo mambo siyajui kabisa kabisa. Tangu nizaliwe na kuja hapa Chimara sijawahi kufika kwenye mashamba ya wanakijiji hao, mimi sifanyi biashara yoyote ni askari tu na huyo Atanasi Yusuph Yawanga ndiyo kwanza namsikia kwako, simfahamu kabisa mtu wa aina hiyo,” alisema Polisi Mgonja.
Alipoulizwa kuhusu tuhuma za kuwaweka ndani wanakijiji wanaokataa kumpatia debe sita za mpunga kwa kila ekari wanayovuna, pia alikanusha kwa kueleza; “Kama sijafika kwenye hayo mashamba nawawekaje ndani sasa. Na kwanini unaniuliza hayo maswali, kwani hata kama ni kweli si utaandika, haya itasomwa, ndiyo kitabadilika nini?” alihoji.
![]() |
Korokoroni |
Tanzania PANORAMA ilimweleza kuwa yeye kama mlinzi wa raia na mali zao kulalamikiwa kufanya vitendo vya kinyama kwa raia anaopaswa kuwalinda siyo jambo zuri kwake na kwa jeshi analolitumikia lakini alisema yeye ni mtumishi mwaminifu ambaye hajawahi kunyanyasa raia.
Katika hatua ya kushangaza, muda mfupi baada ya kuzungumza na Tanzania PANOIRAMA, Polisi Mgonja alituma pesa kwenye simu akitumia laini ya simu yake nyingine ambayo ilisomeka jina lake na alipopigiwa kuulizwa pesa alizotuma ni za kazi gani alisema alikuwa anajaribu kutuma.
Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Mbeya (RPC), Ilrich Matei alipoulizwa hilo alisema hakuna askari polisi anayekatazwa kufanya biashara ya aina yoyote ilimradi havunji sheria za nchi.
Alisema tuhuma dhidi ya Polisi Mgonja hajawahi kuzisikia wala hazijafika kwake na aliwataka wanakijiji hao kwenda kumuona kumfikishia malalamiko yao ili aone kama kuna makosa ya jinai afungue jalada la uchunguzi.
“Polisi yeyote anaruhusiwa kufanya biashara ilimradi havunji sheria za nchi. Lakini kama huyo polisi wangu anafanya mambo ya kinyama mimi sijafikishiwa taarifa zake. Hao wanakijiji waambie waje kwangu niwasikilize ili nifungue jalada la uchunguzi ili kubaini kama kuna jinai basi nitachukua hatua haraka.
“Mara nyingi raia huwa wanaogopa tu wakiona askari basi wanabaki wananyanyasika lakini polisi ni mtu kama wao. Mimi ni mtu mzima katika kazi hii wala sitaki kumkingia kifua mtu, nasema kama kuna jinai naomba niletewe nichukue hatua. Na hata hawa askari wangu huwa nawaambia kuna maisha nje ya uaskari hivyo waishi vizuri na raia,” alisema Kamandsa Matei.
Jitihada za kumtafuta John Shillinde anayedaiwa kupokwa kandarasi ya mradi huo na kudhulumiwa fedha alizotumia katika ujenzi wa banio hazikufanikiwa.
Hata hivyo, wakati Polisi Mgonja akikanusha kuhusika na sakata hilo, Tanzania PANORAMA imebaini kuwepo kwa wajumbe watatu wa wakulima wa Kijiji cha Iyala waliowekwa ndani wakishinikizwa wawalazimishe wakulima wa kijiji hicho wamlipe Polisi Mgonja debe sita za mpunga kwa kila ekeri waliyovuna.
Aidha, taarifa zaidi zilizopatikana kutoka serikali ya kijiji hicho zimeonyesha kuwa uongozi wa kijiji upo katika shinikizo la kulazimishwa uandike barua ya kukubali wakulima wa kijiji hicho kulipa sehemu ya mazao yao kwa Polisi Mgonja.
Tanzania PANORAMA Blog inaendelea kufuatilia sakata hili na italiripoti kwa kina, hatua kwa hatua.
Acheni kuchafua watu nyie nakablog kenu uchwara endeni tuna mjua no Askari anaeishi na watu vizuri Sana hapa chimala no mtu wawatu mmepiga pesa mumchafue watu na story za kutunga Kama wanaonewa si wangeenda mahakamani acheni kuchafua watu hili mpate followes
Mnatetea msichokijua kama anaonewa na kuchafuliwa mtajua mbele