Monday, June 9, 2025
spot_img

JINSI WAFANYAKAZI BENKI NMB WANAVYODAIWA KUIBA NA KUREJESHA FEDHA ZA WATEJA

RIPOTA PANORAMA

MBINU inayodaiwa kutumiwa na wafanyakazi wa Benki ya National Microfinace Bank (NMB) kuiba fedha kwenye akaunti za wateja kisha kuzirejesha wanapobainika, imefichuliwa.

Aliyefichua mbinu hiyo ni Habakuki Stefano Nsyenge ambaye amefanya mahojiano na Tanzania PANORAMA Blog wiki hii, jijini Dar es Salaam akielezea madai ya kuibiwa fedha zake kwenye akaunti na wafanyakazi wa benki hiyo, kisha kurejeshewa huku akiombwa msamaha na Meneja wa Benki ya NMB Tawi ka Mafinga, Focus Lubembe.

Katika mahojiano hayo, Nsyenge anadai alibaini fedha zake zimeibiwa kwenye akaunti baada ya kuangalia bank statement yake na kubaini akaunti yake ya mkulima inakatwa ‘service charges’ mara mbili ambazo ni ‘saving na ‘current.’

Akielezea jinsi alivyobaini hilo wakati wa mahojiano hayo, kwa maneno yake mwenyewe, Nsyenge anadai; “Yule mhudumu wa benki alipoangalia kwenye akaunti yangu, ‘psychologically’ nikaona anashtuka. Baadaye ninapongoja majibu nikaona hana majibu ya kunipa na wakati huo huo kwenye dirisha lake kukawa kuna mstari mrefu wa wateja wanangoja. Mimi nikamwambia kijana naona hii ni ‘technical issue’ naomba niruhusu uendelee na wateja wengine mimi nitakuja kesho.

“Kwa hiyo tukaachana pale nikamfuatilia kesho yake, lakini ninapomfuatilia kesho yake sikwenda kwa maneno, nilikuwa nimeishaandika barua kabisa inayoonyesha mazingira ya akaunti yangu ni nini nimechukua na kile ambacho kinapungua kwenye akaunti yangu. Bahati nzuri kesho yake nilimkuta yule yule mhudumu nikampatia ile barua akaipeleka kwa supervisor wake.

“Ilipopelekwa kwa supervisor, ninaposubiri majibu, supervisor naye akakosa majibu. Baada ya kukosa majibu akanambia samahani baba naomba uniachie namba yako ya simu nitakupigia baada ya siku kadhaa, siku mbili, tatu. Nikampa namba yangu ya simu, ilikuwa nafikiri ijumaa, jumamosi ikawa kimya, jumatatu ikawa kimya, jumanne mimi nikaenda lakini bado akawa hana majibu ya kunipa.

“Baadaye mimi nikalazimika kuingia na kuangalia kwenye ‘bank statement’ yangu ili nione uhalisia maana kabla ya hapo nilikuwa sijaangalia, sasa nilipo ‘check’ kwenye ile ‘statement’ ndipo sasa nikaona kwanini kuna kigugumizi katika suala la akaunti yangu.

“Nilipo ‘check’ nikagundua kuna makato ambayo yameandikwa kwa namna ambayo mtu mwingine asiyejua, anaweza kuona ni ya kawaida. Lakini ikaonekana makato yanaandikwa, ‘service charges, savings and current.’ Sasa nikajiuliza toka lini akaunti moja ikawa inasomeka ‘savings and current,” alidai Nsyenge.

Akizungumzia zaidi jinsi alivyofuatilia suala hilo, Nsyenge anaendelea kudai kuwa alimtafuta mwanasheria ambaye baada ya kuangalia ‘bank statement’ yake alimwelekeza kumwandikia barua Meneja wa NMB Tawi la Mafinga kuyahoji makato hayo kwenye akaunti yake.

Anadai baada ya kumkabidhi meneja barua, aliwasiliana na ‘supervisor’ naye akakiri kuona barua ya malalamiko yake na kwamba wawili hao walishauriana kwa muda kabla ya kumuomba awape muda wa kushughulikia tuhuma alizokuwa akiielekezea benki hiyo.

“Nilipokwenda kuonana na meneja baada ya kuniomba niende, nilimwambia mazungumzo yangu yata ‘base’ katika mambo kadhaa ambayo itabidi tuyazungumze tuone tunatoka vipi. Moja nilitaka wafahamu wamesababisha hela yangu kuchelewa kutoka na kunivurugia shughuli zangu lakini pili wamenisababisha mateso kisaikolojia.

“Lakini hapo hapo kuna maswali ambayo nilipowauliza hawakunijibu. Nilipowauliza maswali hawakunijibu. Nikawaambia nimewasiliana na mwanasheria wangu naye kanishauri kabla sijachukua hatua nyingine nionane nao ili kama tutaelewana kwa yale ninayohitaji nitachukua haki zangu na kuwaacha waendelee na shughuli zao lakini tofauti ya hapo, itabidi nichukue hatua nyingine za kisheria.

“Tulizungumza tukaelewana, nilipokwenda tena wakasema wanaomba niwasamehe sana sana kwa hayo waliyoyafanya……. Mimi nisiwe kisababishi cha wao kufukuzwa kazi maadamu wameishajua watu wao wanafanya hivyo vitu, maana yake wamekuwa wanawaibia wateja kwa namna mbalimbali na bahati mbaya wengi hawajui… hawajui zile lugha za kibenki za miamala.

“Niliwaambia ni rahisi watu wasiojua lugha za kibenki kuibiwa na inaonekana hayo ndiyo mazoea ya benki hiyo kuwaibia wateja lakini kwa bahati, kwangu imefika imegonga mwamba, nimewagundua ndiyo maana ninawafuatilia.

“Kwa hiyo mimi sikuwa na neno ila niliwaambia wanachotakiwa kufanya ni kunirudishia hela yangu lakini pia kulipa gharama, advance niliyokuwa nimeipeleka kwa wakili ili mimi, baada ya hapo nifunge akaunti yangu niachane nao kama benki kwa sababi ‘its useless’ kufanya na watu ambao hawawezi kuheshimu maadili ya taasisi yao,” alidai Nsyenge.

Anaendelea kudai zaidi kuwa vijana waliohusika kutenda tukio hilo meneja aliwaita ofisini kwake akawataka warudishe fedha walizokuwa wamezichukua kwa njia hiyo ya makato na kulipa fedha ambazo Nsyenge alikuwa amemlipa wakili kama advance ya kusimamia shauri lake.

Nsyenge anadai vijana hao walilipa sehemu ya fedha zake na kwamba badala ya kuzirudisha kwenye akaunti yake wamekuwa wakimlipa mkononi kwa mafungu na hadi sasa bado hawajamaliza kumlipa kiasi cha fedha walizokubaliana.

PANORAMA imemuuliza Kaimu Meneja Habari na Mawasiliano wa NMB, Vicent Mnyanyika kuhusu malalamiko hayo ya kukatwa ‘service charge’ mara mbili (saving na current) katika akaunti moja naye akijibu, alisema hawezi kujibu kila malalamiko inayoelekezewa benki ya NMB.

Pamoja na mambo mengine, Mnyanyika alielekeza PANORAMA kujiongeza kujua taasisi za benki zinavyoendeshwa na jinsi mambo ya akaunti yalivyo na alipoelezwa kuwa wajibu wa kuelimisha umma kupitia vyombo vya habari kuhusu shughuli za kibebnki ili kuwapa wananchi uelewa ni wake kulingana na wadhfa aliokasimiwa kwenye taasisi hiyo unaompa mamlaka ya kuwa msemaji wa NMB, alisema kwa mteja ambaye hajaenda NMB kulalamika, yeye hawezi kusema lolote.

Alipoulizwa iwapo kwa wadhfa wake kama Kaimu Meneja Habari na Mawasiliano wa NMB hawezi kutoa ushirikiano kwa vyombo vya habari vinavyomfikia kuomba ufafanuzi au kauli ya NMB kuhusu mambo yanayohusu taasisi hiyo alisema yuko njiani anaendesha gari atafutwe jumatatu, saa nne asubuhi.

Mnyanyika ametoa kauli hii sasa, wakati viongozi wa Serikali wakiwemo viongozi wakuu wa kitaifa wakisisitiza maafisa habari wa Serikali na taasisi za umma kutekeleza ipasavyo wajibu wao wa kupasha habari umma na kushirikiana na vyombo vya habari kikazi, na hasa kutoa ufafanuzi wa mambo ambayo wananchi wanayahoji.  

ENDELEA KUSOMA TANZANIA PANORAMA ILI KUJUA ZAIDI KUHUSU SAKATA HILI.      

Nyingine Zinazohusiana na Hii

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Tufuatilie

0FansLike
3,913FollowersFollow
0SubscribersSubscribe
- Advertisement -spot_img

Habari Nyingine Mpya