MWANDISHI MAALUMU
WADAU wa lishe wameaswa kuunga mkono jitihada za serikali kupambana na changamoto za lishe wakati Tanzania ikijiandaa kufanya mkutano mkuu wa 11 wa wadau wa masuala ya lishe.
Rai hiyo imetolewa na jana na Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Chakula na Lishe, Dk. Germana Leyna alipokuwa akihojiwa na Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC), jijini Dar es Salaam.
Dk. Leyna alisema Tanzania imepiga hatua kubwa katika kukabiliana na changamoto za lishe kwa sababu ya mikakati madhubuti iliyojiwekea.
“Serikali imeendelea kuweka mikakati mbalimabli ikiwemo kuendelea kutoa elimu kwa umma na kuhakikisha jamii inakuwa na uelewa wa masuala ya lishe ili kuendelea kuwa na taifa lenye watu wenye lishe bora.

Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Chakula na Lishe, Dk. Germana Leyna.
“Niseme hapa kuwa wadau waje tunganishe nguvu katika kupambana na changamoto za maswala ya Lishe,” alisema Dk Leyna.
Alisema serikali itahakikisha inawafikia wazalishaji hasa wakulima wawapo katika shughuli zao za kilimo ili kuwapa elimu ya lishe bora na umuhimu wa kutunza chakula kwa ajili ya matumizi ya nyumbani badala ya kuuza chote.
Dk. Leyna alisema wadau wanapaswa kuendelea kujitokeza na kuweka chachu katika masuala ya lishe nchini.


