ZERUBABEL CHUMA
SERIKALI za Tanzania na India zinakusudia kuimarisha ushirikiano katika sekta ya ulinzi.
Hayo yamesemwa juzi na Makamu wa Rais, Dkt. Philip Mpango alipokuwa akizungumza na Naibu Waziri wa Ulinzi wa India, Sanjay Seth, Ikulu Dar es Salaam
Dkt. Mpango alisema ziara aliyofanya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan nchini India, Oktoba 2023 imeimarisha zaidi uhusiano uliopo.
Alisema ushirikiano unaokusudiwa ni kubadilishana mafunzo ya kijeshi na viongozi wa Wizara za Ulinzi wa Tanzania na India kutembeleana.
Alipongeza zoezi la pamoja la kijeshi la nchi hizo mbili na nchi washirika kutoka Afrika lililohusisha Jeshi la Wanamaji na maonesho ya zana na vifaa vya ulinzi.
Alitaja maeneo mengine ambayo Tanzania inashirikiana na India katika masuala ya ulinzi kuwa ni mafunzo ya pamoja ya kijeshi ya kudhibiti ugaidi, kupambana na uharamia, uokoaji na doria za pamoja.
Aidha, alipongeza ushirikiano uliopo kwa nchi hizo mbaili katika masuala ya afya, elimu, Maji, usafiri na huduma zingine za kijamii.

Nibu Waziri wa Ulinzi wa India, Sanjay Seth na ujumbe wake, alipokutana na kuzungumza na Makamu wa Rais, Dkt Philip Mpango, Ikulu, Dar es Salaam.
Kwa upande wake Naibu Waziri wa Ulinzi wa India, Sanjay Seth alisema Tanzania imeimarisha zaidi ushirikiano na India na hivi sasa ni mshirika wa kuaminika katika sekta mbalimbali za kiuchumi na kijamii ikiwemo biashara, uwekezaji, maji, afya na elimu.
Sanjay alisema Tanzania ni nchi ya pili barani Afrika kwa ufanyaji biashara na India ikitarajiwa kufikia Dola za Marekani, bilioni nane mwaka 2024/2025.
Mazungumzo hayo yalihudhuriwa na Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Balozi Dkt. Stergomena Tax, Balozi wa India nchini Tanzania, Bishwadip Dey pamoja na viongozi mbalimbali wa Jeshi la Ulinzi kutoka Tanzania na India.
