ZERUBABEL CHUMA
KIKOSI maalumu chenye askari 27 kutoka taasisi zinazounda Jeshi la Uhifadhi kimewadhibiti fisi waharibifu 25 waliokuwa wakihatarisha usalama wa wananchi wa Mkoa wa Simuyu.
Mkurugenzi wa Kitengo cha Uratibu wa Jeshi la Uhifadhi, Kamishna Msaidizi Mwandamizi (SACC), Fidelis Kapalata amewaambia waandishi wa habari kuwa kudhibitiwa kwa fisi hao ni hatua za makusudi zinazochukuliwa na Wizara ya Maliasili na Utalii za kukabiliana na wanyama waharibifu.

Mkurugenzi wa Kitengo cha Uratibu wa Jeshi la Uhifadhi, Kamishna Msaidizi Mwandamizi (SACC) Fidelis Kapalata.
Akizungumza na waandishi wa habari jana mkoani Dodoma, Kapalata alisema Wizara ya Maliasili na Utalii imeongeza nguvu za kukabiliana na wanyama wakali na waharibifu na hasa fisi ambao wamekuwa wakiwasumbua wananchi katika maeneo mbalimbali nchini.
Alisema kazi ya kukabiliana na wanyama wakali na waharifu wanaoingia kwenye makazi ya watu imefanywa na kikosi maalumu cha Jeshi la Uhifadhi kikishirikiana na Serikali za Halmashauri za Wilaya za Mkoa wa Simiyu.
“Napenda kutoa shukrani na pongezi kwa askari wetu waliopo uwandani, wananchi na Serikali za Wilaya za Mkoa wa Simiyu kwa kazi nzuri iliyofanyika ya kuwakabili wanyamapori wakali na waharibifu.
“Niendele kuwaomba wananchi kuendelea kushirikiana na askari wetu katika kazi hii ili tuweze kufikia malengo yanayokusudiwa,” alisema Kapalata

Askari wa Kikosi Maalumu cha Jeshi la Uhifadhi cha kupambana na wanyama wakali na waharibifu wakiwa kazini.
Aidha, Kapalata alisema hivi karibu kumeripotiwa uwepo na fisi waharibifu katika Kambi ya Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) iliyopo Wilaya ya Kongwa, Mkoa wa Dodoma.
Alisema tayari wizara imechukua hatua ya kupeleka kikosi kazi cha askari ambao wameweka kambi huko na kazi ya kuwasaka fisi hao imeshaanza.
“Kuhusu taarifa ya uwepo wa fisi hatarishi katika Kambi ya Jeshi la Kujenga Taifa Wilaya ya Kongwa, tumeshapeleka askari wetu nao wameanza kazi ya kuwasaka fisi hao. Ni imani yetu tutaitokomeza changamoto hiyo kwa mafanikio kama ilivyokuwa katika Mkoa wa Simiyu,” alisema Kapalata.