Saturday, June 14, 2025
spot_img

MASOUD KIPANYA AMSHIKA PABAYA MWIJAKU

RIPOTA PANORAMA

MCHORA katuni maarufu Afrika, Ally Masoud Nyomwa, maarufu zaidi kwa jina la Masoud Kipanya anakusudia kumshtaki mahakamani Burton Mwemba Mwijaku kwa kumkashifu na kuandika habari za uongo dhidi yake katika ukurasa wake wa mtandaoni wa facebook.

Kipanya amempa siku tatu Mwijaku kuomba radhi kwa uzito ule ule aliotumia kumchafua sambamba na kumlipa Shilingi 5 bilioni kama fidia.

Kwa mujibu wa barua ya Wakili wa Kipanya, Wakili Msomi Mwandamizi wa Kampuni ya Haki Kwanza Advocates, Alloyce Komba ya Juni 7, 2024, inamwelekeza Mwijaku kujitafakari na kuomba radhi kwa maandishi kupitia mitandao yote aliyotumia sambamba na kulipa Shilingi 5 bilioni kama fidia ya kumdhalilisha mitandaoni  Kipanya.

Wakili Msomi Mwandamizi wa Kampuni ya Haki Kwanza Advocates, Alloyce Komba

Barua ya Wakili Komba kwenda kwa Mwijaku ambayo Tanzania PANORAMA Blog imeiona, inaeleza kuwa Juni 4, mwaka huu akitumia ukurasa wake wa  facebook wenye nambari 108657908847651 na kwenye akaunti yake ya Instagram, aliandika mambo ya uongo, nia mbaya na uzushi dhidi ya Kipanya ambaye ni mfanyabiashara, mwanahabari kitaaluma, Muislam mcha Mungu na aliyejenga heshima yake kwa jamii kwa zaidi ya miaka 30.

Barua hiyo inanukuu alichoandika Mwijaku kwenye kurasa zake za mitandoani na kusambaa kwenye mitandao mingine kuwa; ‘nakuheshimu Masuod Kipanya@ masoud kipanya au unataka woote tufanye biashara haramu kama unazo fanya wewe?

‘Wengine hatuwezi kufanya biashara haramu kama wewe mzee, mimi ninatafuta hela yangu ya halali mzee, sijawahi kula pesa haramu kama wewe.

‘Kaa utubu dhambi zako na hayo mabiashara yako ya kiharamu mzee, laiti watanzania wangejua unayoyafanya, sidhani kama kuna mtu angeketi kukaa na wewe au hata kuzungumza na wewe.

‘Umekuwa mwiba kwa vijana kuharibikiwa maisha yao na hakuna aliyesimama na kukunyooshea kidole na kujiingiza kwenye mabiashara yako haramu, hakuna aliyekusema wala kukushauri.

Ally Masoud Nyomwa, maarufu zaidi kwa jina la Masoud Kipanya

‘Kama ulizoea kuwazodoa viongozi wa nchi na marais kwa kuwadhalilisha, sio mimi, sitakaa kimya. Ungekuwa mtangazaji bora usingekubali kuhongwa ili uiseme vibaya serikali na viongozi wake.

‘Na unajua kabisa ni kosa kutumika hivyo, na watu wamekaa kimya kabisa na serikali imeamua kukupuuza.’

Barua hiyo inaeleza kuwa Kipanya amesikitishwa na taarifa hizo zisizo kuwa na ukweli kwa sababu hajawahi kufanya biashara haramu zinazoharibu maisha ya vijana na kwamba andiko limeenda mbali zaidi likimtuhumu kuhongwa ili kuichafua serikali na viongozi wake.

Inazidi kueleza kuwa Kipanya ni mchora katuni maarufu Tanzania, Afrika na duniani kwa ujumla; ni muislamu mzuri hivyo taarifa zilizoandikwa na Mwijaku kwenye kurasa zake mitandaoni zimeharibu sifa yake mbele ya jamii, wazazi na familia yake.

Barua hiyo inamuelezea Kipanya kuwa mtu aliyejenga heshima yake kwa jamii kwa zaidi ya miaka 30, mtangazaji wa redio na televisheni, mtu anayefanya kazi na mashirika mbalimbali ya kimataifa na pia mwenye wafuasi wengi mitandaoni hivyo andiko la Mwijaku limeharibu taswira na jina lake na pia limechafua rekodi yake mbele ya wazazi wake, familia, mashabiki na umma kwa ujumla.

Inahitimisha kwa kueleza kuwa Kampuni ya Haki Kwanza Advocates inayo maelekezo ya Kipanya ya kumpa siku tatu Mwijaku, kuanzia siku aliyopokea barua hiyo kuomba radhi na kulipa Shilingi 5 bilioni kama fidia na iwapo hilo halitafanyika, hatua za kisheria zitachukuliwa dhidi yake.

.

Nyingine Zinazohusiana na Hii

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Tufuatilie

0FansLike
3,913FollowersFollow
0SubscribersSubscribe
- Advertisement -spot_img

Habari Nyingine Mpya