MWANDISHI WETU – WHMTH,
Arusha
SERIKALI ya Tanzania imeahidi kuendelea kushirikiana na Umoja wa Posta Duniani (UPU) na mashirika mengine ya kimataifa kukuza na kuendeleza Malengo ya Maendeleo Endelevu (SDGs) na ustawi wa jamii yote ulimwenguni.
Ahadi hiyo ilitolewa jana, Juni 13, 2024 na Naibu Katibu Mkuu wa Wazira ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Nicholas Merinyo Mkapa alipokuwa akitoa hotuba ya kufungua mkutano wa kikanda wa mkakati wa dunia wa maendeleo ya Posta kwa Afrika
Mkapa ambaye alimwakilisha Naibu Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mhandisi Maryprisca Mahundi kwenye mkutano huo, alisema Tanzania imejitoa kwa dhati kuhakikisha Sekta ya Posta inaendelea kuwa na manufaa na kuchangia kukuza na kuimarisha uchumi wa Nchi za Afrika.
“Tanzania inajitoa kwa dhati kuhakikisha Sekta ya Posta inaendelea kubaki yenye manufaa na kuchangia kwa kiasi kikubwa kukuza na kuimarisha uchumi wa nchi zetu,” alisema Mkapa.
Aidha, washiriki wa mkutano huo na wadau wa Sekta ya Posta kutoka Afrika na duniani, wametakiwa kujitoa kwa dhati kufanya kazi ya kujadili mkakati wa Umoja wa Posta duniani 2026-2029 unaohusika na maendeleo ya Sekta ya Posta na kuutekeleza kwa moyo, uwajibikaji na kwa ushirikiano.

Wajumbe wa mkutano wa kikanda wa kujadili mkakati wa dunia wa maendeleo ya Posta wa mwaka 2026-2029 kwa Afrika wakisikiliza hotuba ya mgeni rasmi (hayupo pichani). Mkutano huo unafanyika Jijini Arusha.
“Mchango wenu katika mkutano huu ni muhimu katika kuhakikisha kuwa majadiliano yenu yanakuwa na matokeo chanya, yatakayokuja na mpango mkakati utakaotuongoza kwa wakati ujao,” alisema Mkapa.
Alisema ana uhakika siku mbili za mkutano huo zitaainisha mtazamo wa pamoja wa kuanzisha mkakati imara utakaoiweka Sekta ya Posta mbele ya mawasiliano na biashara duniani na kwa namna ya pekee, ukanda wa Afrika.
Awali, Salome Kessy aliyemwakilisha Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Mohammed Khamis, akimkaribisha mgeni rasmi kufungua mkutano huo, alisema muda wa siku mbili za mkutano huo zitawapa fursa wajumbe kujadiliana kwa kina na kutoa mapendekezo yanayooanisha mikakati ya kikanda na mwenendo na uvumbuzi wa Posta Duniani.
Alisema mambo makuu yanayolengwa katika mkutano huo ni uimarishaji wa utoaji huduma, matumizi ya teknolojia mpya na kuhakikisha huduma za Posta Afrika zinakuwa endelevu na himilivu.
Mkutano wa kikanda wa kujadili mkakati wa dunia wa maendeleo ya Posta wa mwaka 2026-2029, kwa Afrika unaosimamiwa na Umoja wa Posta Duniani UPU utahitimishwa Juni 14, 2024 kwa maazimio yatakayoisaidia sekta hiyo kusonga mbele kwa mafanikio.
MATUKIO KATIKA PICHA, MKUTANO WA KIKANDA WA KUJADILI MKAKATI WA DUNIA WA MAENDELEO YA POSTA WA MWAKA 2026-2029 KWA AFRIKA. MKUTANO HUO UNAFANYIKKA JIJINI ARUSHA






