RIPOTA WA WAZIRI MKUU
Uvinza, Kigoma
WAZIRI Mkuu, Kassim Majaliwa amesema kama Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan anafanya ziara na kusilikiliza kero za wananchi, haoni ni kwa nini watumishi wengine wa umma wanashindwa kufanya hivyo.
Akizungumza na wananchi na watumishi wa halmashauri na wananchi wa Uvinza, Alhamisi, Septemba 21, 2023 kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika katika viwanja vya Shule ya Msingi Nguruka, wilayani humo, Majaliwa alisema viongozi wanapaswa kutenga siku tatu katika wiki kwenda kuwasikiliza wananchi.
.“Iwapo mkuu wa nchi, Rais wetu Samia Suluhu Hassan anaenda kote nchini na kusikiliza wananchi, je ninyi ni akina nani? Nilishasema mtenge siku tatu katika wiki mwende vijijini na kuwasikiliza wananchi.Â
“Mheshimiwa DC simamia watu wako waende vijijini. Nilishasema hata kama magari ni machache, pangeni ratiba, mbebane na mwende kuwasikiliza wananchi. Gari litawapeleka na kuwaacha kwenye vijiji husika na wakati linarudi litawapitia wote. Nenda mkawasikilize wananchi, nenda mkawatumikie wananchi,” alisisitiza Majaliwa.
Aidha, alisema Serikali itatoa Sh. milioni 500 za kujenga kituo kipya cha afya katika Tarafa ya Nguruka, wilayani Uvinza mkoani Kigoma.
Hayo aliyasema akiwa katika mkutano wa hadhara uliofanyika katika viwanja vya Shule ya Msingi Nguruka.
Majaliwa alisema uamuzi huo ufikiwa baada ya ombi la Mbunge wa Kigoma Kusini, Nashon Bindyaguze ambaye amekuwa akilalamikia udogo wa kituo kilichopo ikilinganishwa na idadi ya wakazi wa kata nne zilizopo.
“Mbunge wenu amekuwa akilalamikia udogo wa kituo cha afya kilichopo kwamba kinahudumia watu wengi kuliko uwezo wake. Nimeenda kukikagua, baadhi ya majengo yamechakaa, nimeelezwa zamani ilikuwa ni zahanati,” alisema Majaliwa.