Monday, June 9, 2025
spot_img

WAZIRI MKUU AZINDUA JENGO LA EMD RUANGWA

*Ahimiza ulinzi wa vifaa na majengo

RIPOTA WA WAZIRI MKUU

Ruangwa, Lindi

WAZIRI Mkuu, Kassim Majaliwa amezindua jengo la wagonjwa wa dharura kwenye Hospitali ya Wilaya ya Ruangwa ambalo limegharimu Shilingi milioni 390.  

Akizungumza na wakazi wa Ruangwa waliofika kushuhudia uzinduzi huo leo, Majaliwa amesema ameridhishwa na ujenzi huo na hasa kwa vile amekuta kuna vifaa vya kisasa.

“Yote haya ni matunda ya kazi nzuri inayofanywa na Rais wetu, Mheshimiwa Dk. Samia Suluhu Hassan na yamesaidia kuifanya wilaya yetu iwe miongoni mwa wilaya zinazoenda kwa kasi,” amesema.

Majaliwa amesema hospitali hiyo imejengwa kwenye eneo lenye ukubwa wa ekari 100 ambalo kazi ya kujenga uzio ni kubwa hivyo amewataka wakazi hao wawe walinzi wa miundombinu na vifaa tiba vilivyonunuliwa ili waendelee kupata huduma bora na za uhakika.

“Eneo hili lina ekari 100. Ninaomba sana sisi tuwe walinzi wa vifaa hivi vilivyopo hapa ndani na kamwe tusishiriki mpango wowote wa kurudisha maendeleoa nyuma,” amesisitiza.

Naye, Naibu Waziri wa Afya, Dk. Godwin Mollel amesema Serikali imetoa Shilingi bilioni 51.4 kwa ajili ya ujenzi wa hospitali za Taifa na Kanda katika kipindi cha mwaka mmoja.

“Kwa ajili ya hospitali za mikoa nchi nzima, Rais wetu ametoa Shilingi bilioni 54.2 na kwenye eneo la vifaa, ndani ya mwaka huu mmoja ametoa shilingi bilioni 290.9,” amesema.

Naye Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Dk. Festo Dugange amesema jengo hilo ni miongoni mwa majengo 80 yaliyojengwa nchini kwa kutumia fedha za UVIKO-19. Katika mkoa wa Lindi, majengo kama hayo yamejengwa pia katika Wilaya za Liwale na Kilwa.

Amesema katika awamu ya kwanza, wilaya hiyo ilipokea Shilingi bilioni 2.9 ambazo majengo yake yamekamilika na pia imepokea Shilingi milioni 800 za kujenga wodi za kisasa ambazo zitakuwa na vifaa vya kisasa pia.

Mganga Mkuu wa Wilaya ya Ruangwa, Dk. Salvio Wikesi yeye amesema mradi huo  unatarajiwa kuwa na majengo 22 ambayo hadi kukamilika kwake yanatarajiwa kugharimu Shilingi bilioni 7.5.

“Hospitali  inaendelea na ujenzi wa majengo matano ya awamu ya tatu ambayo ni jengo la huduma za dharura, jengo la upasuaji, jengo la kuhifadhia maiti, jengo la wodi ya upasuaji wanaume na wodi ya upasuaji wanawake.

“Hadi sasa, mradi umegharimu Shilingi milioni 390.72 ikiwa ni ongezeko la vifaa na kiasi cha Shilingi milioni 90.72 ambazo zimetumika kuimarisha eneo la hospitali kwa kuwa lilikuwa na maji mengi chini ya ardhi hivyo maandalizi ya ujenzi kuanzia hatua ya msingi hadi jamvi yalihitaji uimarishaji msingi wa jengo,” amesema.

Amesema pamoja na ukamilishaji wa jengo hilo, Serikali pia ilitoa vifaa tiba vya kisasa na Wizara ya Afya ilipeleka mashine ya x-ray, mashine ya kutakasia vifaa kabla ya kufanya upasuaji na mashine ya kumfanyia uangalizi mgonjwa wakati wa upasuaji.

Nyingine Zinazohusiana na Hii

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Tufuatilie

0FansLike
3,913FollowersFollow
0SubscribersSubscribe
- Advertisement -spot_img

Habari Nyingine Mpya