RIPOTA PANORAMA
SERIKALI iko mbioni kuandaa tamasha kubwa la muziki na sanaa litakalofahamika kwa jina la moja ya vivutio vikubwa vya utalii vilivyopo hapa nchini.
Akizungumza wiki hii jijini Dar es Salaam na wadau wa sanaa na muziki, Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dk. Hassan Abbas amesema kwa kutambua urithi mkubwa wa sanaa uliopo nchini ukiwemo muziki, filamu, ngoma na uga mwingine, Serikali kwa kushirikiana na wadau, itaratibu tamasha kubwa la aina yake litakalofanyika baadaye mwaka huu.
Dk. Abbas alisema sekta hiyo inapaswa kuhakikisha inaiburudisha jamii ya watanzania wachapakazi ipasavyo na kwamba sambamba na kuandaliwa kwa tamasha hilo, pia Serikali kwa kushirikiana na wadau itarejesha tuzo za muziki na sekta nyingine zilizo chini ya wizara inayoiongoza..
“Moja ya kazi kubwa ya sekta ya sanaa nchini ni kuhakikisha jamii yetu inayochapa kazi sana kwa sasa inaburudika ipasavyo, sasa naona sanaa inakuja tu pale panapokuwepo mdhamini au mwandaaji fulani, asipokuwepo hakuna matukio na nchi iko kimya.
“Serikali sasa inakwenda kuchechemsha sekta hii kwa kuratibu tamasha kubwa sana litakaloanzia Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam na kuendelea kuungana na tamasha la kimataifa la sanaa Bagamoyo
“Tusisubiri wadhamini, wakija sawa kama wako likizo basi mimi nasema sisi wenyewe tunaweza kwa umoja wetu sasa tukutane Uwanja wa Uhuru Disemba 26, mwaka huu na kisha Disemba 27 twende Bagamoyo.
“Wasanii wakiungana watajaza uwanja, twende tutateremsha wasanii wetu wote ambao ni urithi wa sasa na baadaye wa nchi hii halafu tuone kama watu hawatakuja,” amesema Dk. Abbas.
Dk. Abbas yupo katika ziara ya kikazi ya kukutana na wadau mbalimbali wa sanaa na sekta nyingine zilizo chini ya wizara yake
0711 46 49 84