![]() |
MWANDISHI MAALUMU
LOLIONDO.
WAZIRI wa Mambo ya Ndani ya Nchi. Hamad Yusufu Masauni ameitaka Idara ya Uhamiaji nchini kusimamia uingiaji na utokaji wa wageni katika mipaka ya nchi kwa kufuata sheria za nchi.
Waziri Masauni aliyasema hayo mapema wiki hii akiwa Ngorongoro mkoani Arusha alikokwenda kukagua maendeleo ya kazi ya uwekaji wa alama za mipaka katika eneo la Pori Tengefu la Loliondo.
Aidha, Masauni alibainisha kuwa Serikali itafanya uhakiki wa kina kubaini uendeshaji wa asasi za kiraia nchini kufanya kazi zao kwa mujibu wa sheria na zile zitakazokiuka zitachukuliwa hatua kali za kisheria.
Masauni alieleza kuridhishwa kwake na maendeleo ya kazi na kuwataka wahusika kuhakikisha kuwa kazi hiyo inakamilika kwa wakati.
Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Ngorongoro Mwalimu Raymond Mangwala aliyemwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Arusha, John Mongela, alimueleza Waziri Masauni kuwa amepokea maelekezo yake na atahakikisha hali ya usalama wa wananchi na mali zao inaendelea kuimarishwa wilayani Ngorongoro na kuwa kazi hiyo itaendelea kwa hali ya amani na utulivu.