Monday, June 23, 2025
spot_img

FAILI TUHUMA ZA NGONO BOSI BANDARI LIPO TAKUKURU

Mkurugenzi Mkuu wa TAKURURU, Salum Hamduni

 

RIPOTA PANORAMA

0711 46 49 84

FAILI la tuhuma za kuomba rushwa ya ngono na unyanyasaji wanawake mahali pa kazi zinazomkabili Mkurugenzi wa Rasilimali Watu wa Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA), Gabriel Mwita Thobias lipo Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU).

Gabriel Mwita Thobias


 

Faili hilo lipo TAKUKURU kwani maafisa wa taasisi hiyo kutoka makao makuu walifanya uchunguzi wa tuhuma hizo dhidi ya Thobias wakati ule, ambapo hata hivyo mpaka sasa inadaiwa limefungiwa kabatini.

Uchunguzi huo ulifanyika wakati ambao Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU hakuwa huyu wa sasa.

Mkurugenzi Mkuu wa sasa wa TAKUKURU, Salum Hamduni alipoongea na Tanzania PANORAMA Blog ameahidi kulifukua faili hilo na kulifanyia kazi.

“Asante kwa taarifa hizi za kuwepo kwa faili hilo katika taasisi yangu, nakuahidi kufuatilia lilipo ili kujua uchunguzi ulipoishia na nitarejea kwako,” alisema.

Uchunguzi uliofanywa na Tanzania PANORAMA Blog umeonyesha kuwa Menejimenti ya Tanzania Leaf Tobacco Company Limited (TLTC), baada ya kupokea ripoti ya kamati ya nidhamu iliyochunguza tuhuma dhidi ya Thobias na kuifanyia kazi, iliripoti tuhuma zake kwa TAKUKURU.

Taarifa zinaonyesha kuwa TAKUKURU makao makuu ilituma timu ya maafisa uchunguzi iliyoongozwa na mtu aitwaye Hazina Mwisho, ambayo ilikwenda Morogoro kufanya uchunguzi huo.

Hata hivyo, katika hali ya sintofahamu, baadaye wachunguzi hao walikutana na aliyekuwa Mkuu wa Mkoa huo, Dk. Stephen Kabwe kabla ya kurejea makao makuu ambako baada ya hapo ukimya ulitawala kuhusu uchunguzi huo.

Taarifa kutoka kwa watu wa karibu zinaonesha kuwa Dk. Kebwe ana  uhusiano wa kindugu na Thobias.

“Tangu mwanzo wa skandali hii kulikuwa na nguvu kubwa sana iliyokuwa inatumika kuizima, kumbuka anayetuhumiwa siyo mtu mdogo, angeweza kufanya lolote, ni mtu mzito haswa na hata kule TLTC ingekuwa ni hivi hivi tu angezima hilo jambo lakini sasa kule kuna wenzetu weupe, wamenyooka na masuala ya unyanyasaji wa kijinsia wanayapiga vita kwa nguvu kubwa.

“TLTC ni kampuni ya kimarekani ni kampuni kubwa yenye matawi 17 katika nchi za Afrika na kwingineko duniani, lakini kwa hapa Tanzania hivi sasa imesimamisha uzalishaji ila wakati wowote wanaweza kuanza uzalishaji.

“Sasa baada ya Thobias kutuhumiwa sana alifikishwa kwenye kamati ya nidhamu ambayo kiongozi wake alikuwa mzungu aitwaye Wayne Kluckow raia wa Afrika Kusini ambaye anafanya kazi katika ofisi ya kanda iliyoko huko na kwa sababu ya uzito wa nafasi aliyokuwa nayo Thobias, wajumbe wote wa kamati hiyo walitoka nje ya nchi hasa wale wanaoshughulikia mambo ya ‘compliance.’

“Kamati ya nidhamu baada ya kusikiliza shauri hilo na mashahidi wote ilimkuta na makosa akafukuzwa kazi na menejimenti ikaripoti tuhuma zake TAKUKURU, nayo ikaunda timu ya wachunguzi kutoka makao makuu waliokwenda Morogoro na kuwahoji walalamikaji na wakurugenzi wa kampuni.”

Alipoulizwa afisa wa TAKUKURU aliyeongoza timu iliyokwenda Mkoa wa Morogoro kufanya uchunguzi, Hazina Mwisho kuhusu kilichobainika kwenye uchunguzi na walichoongea na aliyekuwa Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Kebwe alisema hakumbuki hata kidogo kushiriki uchunguzi huo.

Alipoelezwa kuwa Tanzania PANORAMA Blog inazo taarifa za uhakika za yeye kuongoza timu hiyo na kwamba yeye na timu yake walikutana na Kebwe, alisema; “Nasema sina kumbukumbu hizo, hizo kazi zipo ofisini makao makuuu, kama hiyo kazi ilikuwepo mwelekezaji wa utekelezaji alikuwa Mkurugenzi Mkuu.

“Mimi sipo makao makuu kwa sasa nipo Wilaya ya Temeke. Hizo ‘issue’ za Kampuni ya Tumbaku zilikuwa na maelekezo ya Mkurugenzi Mkuu hicho ndicho ninachokikumbuka sasa wewe wasiliana na makao makuu,” alisema Mwisho.

Kwa upande mwingine, baadhi ya mashahidi waliotoa ushahidi wao kwenye kamati ya nidhamu dhidi ya tuhuma za Thobias walioongea na Tanzania PANORAMA Blog wameeleza kuwa kufukuzwa kwake kazi kulichangiwa na mambo mengi ambayo kamati ya nidhamu iliyabaini wakati ikiendesha shauri lake.

Mmoja wa watu waliotoa ushahidi wa tuhuma dhidi ya Thobias, Gladys Almas ameiambia Tanzania PANORAMA Blog kuwa mbali na tuhuma zinazoripotiwa sasa, alikuwa na mambo mengine mengi yaliyosababisha afukuzwe kazi.

“Sipendi kuyakumbika hayo, sipendi kuyaongelea, yule bwana alikuwa na mambo mengi sana yaliyosababisha afukuzwe kazi siyo hayo tu, sitaki kukumbuka, alisema Gladys.

Shahidi mwingine aliyefika mbele ya kamati ya nidhamu ambaye ameongea na PANORAMA ni Josephine Mworia ambaye alisema Thobias pia alikutwa na makosa na kukiuka taratibu za kazi.

“Mimi niliitwa kama shahidi kwenye kamati na nilieleza yale ya upande wangu. Lakini Thobias alikuwa na mambo mengi mno, alikuwa na matatizo mengi sana kwa mfano mimi nilikuwa katika orodha ya watu wa kupunguzwa kazini na yeye ndiye alikuwa na orodha hiyo kama kiongozi mkuu wa idara ya rasilimali watu akaanza kutangaza kwa watu huko pembeni tulio kwenye orodha ya kupunguzwa. 

“Lakini pia akikuchukia basi hakupi kazi na hilo lilinikuta mimi pia, kwa ufupi iko hivi alikuwa na mambo mengi mno yaliyofanya afukuzwe kazi,” alisema Mworia.

Thobias ambaye kabla ya kufukuzwa kazi TLTC alikuwa Mkurugenzi wa Rasilimali Watu, sasa ni mwajiriwa wa TPA akiwa na wadhifa huo huo wa Ukurugenzi wa Rasilimali Watu na anatuhumiwa kuomba rushwa ya ngono na kuwanyanyasa kingono wafanyakazi wa kike aliokuwa akifanya nao kazi TLTC

Nyingine Zinazohusiana na Hii

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Tufuatilie

0FansLike
3,913FollowersFollow
0SubscribersSubscribe
- Advertisement -spot_img

Habari Nyingine Mpya