RIPOTA PANORAMA
0711 46 49 84
WAKATI Benki ya I&M na Benki Kuu ya Tanzania (BoT) zikiendelea kukaa kimya dhidi ya miamala yenye kutia shaka iliyofanywa na Benki ya I&M, imebainika kuwa zaidi ya Shilingi Bilioni 2 zimetolewa na benki hiyo kama fedha tasilimu na kusombwa kwenye viroba na maboksi.
Taarifa zilizopatikana zinadai kuwa fedha hizo zilikuwa zinaingizwa kwenye akaunti ya mteja ambaye hadi sasa hapatikani katika anuani yake na kwamba kila zilipokuwa zikiingizwa, mteja huyo alikuwa akizitoa mara moja.
Benki ya I&M ambako miamala hiyo imefanyika, ilikuwa ikiidhinisha kuchukuliwa kwa fedha hizo kama pesa tasilimu kila zinapoingizwa na kwa zaidi ya wiki tatu sasa imeshindwa kueleza utaratibu inaotumia kuwalipa wateja wake mamilioni ya fedha tasilimu.
Meneja Biashara na Habari wa Benki ya I&M, Anitha Pallangyo, licha ya kufikiwa ana kwa ana na kutumiwa maswali kwa njia ya barua pepe kama alivyoelekeza ili kulizungumzia suala hilo, mara kadhaa alitoa sababu za kushindwa kutoa kauli, amepata pia kueleza kuwa mabosi wake wanaandaa majibu na mwisho alikata mawasiliano.
Meneja Biashara na Habari wa Benki I&M, Anitha Pallangyo |
Mbali na Benki ya I&M, Benki Kuu ya Tanzania nayo imekaa kimya licha ya kuulizwa utaratibu unaopaswa kufuatwa na mabenki yanapowalipa wateja wake mamilioni ya fedha tasilimu.
Wakati mtiririko wa miamala yenye kutia shaka katika Benki ya I&M ikizidi kubainika na benki hiyo na BoT zikiwa kimya, mtaalamu mmoja wa masuala ya kibenki aliyezungumza na Tanzania PANORAMA Blog kuhusu uingizwa na uchukuaji wa fedha hizo, alisema kwa jicho la nje inajengeka picha ya kuwepo utakatishaji fedha.
Akizungumza kwa sharti la jina lake kuhifadhiwa, alisema hakuna sheria inayokataza mteja kupewa kiasi chochote cha fedha tasilimu anapohitaji kuchukua lakini benki zinashauri mteja kutochukua fedha nyingi mkononi kwa sababu za kiusalama.
“Kwanza siamini kama hao maafisa habari wa BoT, kwa zaidi ya wiki moja sasa hawajatoa kauli yoyote kuhusu suala hili. Kama ni kweli basi kuna tatizo sehemu ndani ya BoT, haiingii akilini. Lakini mimi kama mtaalamu wa mambo ya kibenki, kulingana na hayo maswali yako naweza kusema kwamba mteja ni mfalme kwa hiyo hakuna namna ya kumzuia kuchukua fedha zake anapozihitaji.
“Lakini BoT imeweka utaratibu na niseme siyo BoT tu bali dunia nzima, inashauri mtu asitembee na mamilioni hayo yote ya fedha iwe kwenye viroba, maboksi, mkononi au hata kweli gari na au barabara sababu ya usalama wake. Hakuna Benki inayoweza kuruhusu hilo tena likawa la mfululizo hivyo.
“Ndiyo maana hata ukiwa unasafiri huruhusiwa kuwa na zaidi ya Dola za Marekani 10,000. Hizo ni Shilingi Mil 20 na kidogo tu. Hiyo ni sheria, pesa ni zako lakini kiwango kilichowekwa ni hicho na sababu zipo wazi. Inashauriwa kutumia zaidi mitandao ya malipo ya kibenki kwa miamala ya milioni hayo kama hizo Shilingi Mil. 100 au 200 kwa mkupuo mmoja.
“Lakini sasa kwenye kesi hii, haiingii akili kwa hiyo Benki kuwa inatoa fedha tasilimu kila baada ya siku tatu au wiki au mwezi kwa mteja yule yule na kila zinapoingizwa, sijui zinakotoka huko mteja anakuja anazichukua kama pesa taslimu. Na kuna suala la kodi hapo sasa kwa utaratibu huo sijui kodi inapatinaje hapo. Anyway wao ndiyo wanajua zaidi.
“Inawezekana zipo sababu na Benki ilikwishajiridhisha kwa mteja wao kuchukua kiwango hicho cha fedha zikiwa fedha tasilimu lakini kwa huo mtiririko sidhani. Kama Benki wangeweza kumshauri mteja wao kutumia njia nyingine ya uchukuaji wa kiasi kikubwa hivyo cha fedha kuliko huu. Na kama ni jambo la heri tu sijui kigugumizi cha kulisema kinatoka wapi. Hili jambo kwa jicho la nje, ukilitazama tu linakuonyesha kuwepo kwa utakatishaji fedha,” alisema mtaalamu huyo wa mambo ya kibenki.
Taarifa za hizi karibu zilizoifikia Tanzania PANORAMA Blog zinadai kuwa mbali na zaidi ya Shilingi mil 800 zilizotolewa na Benki I&M zikiwa ni fedha taslimu na kusombwa kwenye viroba na maboksi, fedha nyingine Shilingi bil 1.7 zimetolewa na benki hiyo kwa mtindo huo huo.
Fedha hizo zimetolewa katika muda wa miezi mitatu na akaunti iliyotumika kuingiza na kuchukuliwa kwa fedha hizo ni moja.
Taarifa zinaonyesha kuwa baada ya kufanyika kwa miamala yenye thamani ya Shilingi mil 800 ambazo zilikuwa zikilipwa kama fedha tasilimu, akaunti hiyo ilibaki na salio na Shililingi mil. 100,121,785.64 ambazo nazo hazikudumu kwenye akaunti hiyo kwani zilitolewa Shilingi mil, 100 ambazo zililipwa kama fedha tasilimu.
Wiki moja baada ya kufanyika kwa muamala huo, akaunti hiyo iliingiziwa Shilingi mil. 126,256,000, siku mbili baada ya kuingizwa kwa fedha hizo, Benki ya I&M iliidhinisha kutolewa kama fedha tasilimu, Shilingi mil 126.
Hayo yaliendelea, ambapo siku 14 baada ya kuchukuliwa kwa fedha hizo, akaunti iliyotumika kwenye miamala hiyo iliingiziwa Shilingi mil 145,376,00 na hapo hapo, Shilingi mil tatu, zikiwa fedha taslimu zilitolewa.
Siku mbili baadaye Benki ya I&M iliidhinisha kuchukuliwa kwa fedha tasilimu, Shilingi mil 142,000,000, hizo nazo zilichukuliwa kwa utaratibu ule ule uliokuwa ukitumiwa na mchukuaji ambaye ndiye mmiliki wa akaunti inayohusika na miamala yote hiyo.
Katika mwendelezo huo, fedha nyingine, Shilingi mil 255,560,000 ziliingizwa katika akaunti hiyo baada ya wiki mbili na siku hiyo hiyo Shilingi mil 210,000,000, zikiwa ni fedha tasilimu zilichukuliwa kisha muda mfupi baada ya kusombwa kwa mamilioni hayo, Shilingi mil 45,000,000, fedha taslimu nazo zilichukuliwa kwa utaratibu huo huo.
Ilichukua siku 12 akaunti hiyo kuingiziwa mamilioni mingine ya fedha ambapo ziliingizwa Shilingi mil 267,070,000, ambazo zilitolewa kama fedha taslimu baada tu ya kuingizwa. Siku hiyo hiyo ziliingizwa fedha nyingine Shilingi mil 24,000,000, zikafuatiwa na kiasi kingine cha Shilingi mil. 26,000,000.
Kiasi cha Shilingi mil 50, fedha tasilimu kati ya hizo zilizoiingizwa kwa mikupuo miwili nazo zilichukuliwa hapo hapo na siku sita baadaye akaunti hiyo iliingiziwa Shilingi mil 238,650,000 ambazo nazo zilichukuliwa hapo hapo, zikiwa ni fedha tasilimu.
Taarifa zinazidi kuonyesha kuwa zilipita siku tano za ukimya kisha zikaingizwa Shilingi mil 285,600,000 ambazo zilitolewa hapo hapo kwa mikupuo miwili akilipwa mtu anayetajwa kwa jina la Deepak Patel.
Deepak Patel kwanza alilipwa Shilingi mil 200 kisha akalipwa fedha nyingine Shilingi mil 85.
Kisha, alichukua siku 10 nyingine akaunti hiyo kuingiziwa fedha ambapo ziliingizwa Shilingi mil 108,450,000, kisha zikiangizwa nyingine, Shilingi mil 216,650,000.
Baada ya kuingizwa kwa fedha hizo, Shilingi mil 300 ziliidhinishwa na Benki I&M kutolewa kwa mtindo ule ule wa pesa taslimu na siku iliyofuata zilichukuliwa fedha taslimu Shilingi mil 25,000,000.
Siku tatu baadaye, akaunti hiyo iliingiziwa Shilingi mil 284,960,000 ambazo zilitolewa siku mbili baadaye kwa mikupuo miwili na kwa utaratibu ule ule wa mteja kuchukua fedha tasilimu.
Kwanza zilisombwa Shilingi mil 200 na baadaye Shilingi mil. 85.
Wiki moja baadaye, akaunti hiyo ilipokea Shilingi mil 294,860,000 na hapo hapo, Benki ya I&M ikainidhishwa kuchukuliwa kwa Shilingi mil 150 zikiwa ni fedha tasilimu na siku iliyofuata, benki hiyo ikaidhinisha kiasi kingine cha Shilingi mil 144, 900,000 kuchukuliwa kama fedha tasilimu ambazo zilisombwa kwa utaratibu ule ule.
INAENDELEA…