![]() |
Nembo bandia zinazobandikwa katika nyama |
zinazotengenezwa hapa nchini zikionyesha kuwa zimetengenezwa Kenya
NA MWANDISHI WETU
IMEBAINIKA kuwa Kampuni inayojihusisha na uzalishaji wa nyama ya Farmer’s Choice Limited, yenye makao makuu yake barabara ya Off Kamili, eneo la Kahawa, jijini Nairobi inahujumiwa na baadhi ya wafanyabiashara wanaodaiwa kuwa ni watanzania.
Taarifa zilizoifikia Tanzania PANORAMA Blog kutoka kwa baadhi ya wafanyakazi wa wakala wa Kampuni ya Farmer’s Choice hapa nchini, ambayo ni Kampuni ya Bright Choice Limited zimedai kuwepo kwa udanganyifu wa bidhaa za nyama zinazoingizwa nchini kutoka Kenya.
Kwamba wakala huyo anadaiwa kuzalisha baadhi ya bidhaa za nyama za hapa nchini na kuziwekea nembo ya Kampuni Farmers Choice ya Kenya.
Inadaiwa, wakala huyo, kwa muda mrefu amekuwa akinunua nyama katika machinjio ya Vingunguti, Dar es Salaam na kuzipeleka kiwandani ambako huzikata na kuzifungasha kwa kuigilizia mithili ya zile za Farmer’s Choice ya Kenya.
“Huyu ni wakala wa nyama wa Kampuni ya Farmer’s Choice ya Kenya, yeye anapaswa kuuza tu lakini siyo kuzalisha,” alisema mtoa habari ambaye jina lake limehifadhiwa.
Alisema, hata hivyo Kampuni ya Farmer’s Choice ya Kenya imeleta mwakilishi wake hapa nchini kwa ajili ya kusimamia biadhaa zake zote lakini katika hali ya kushangaza, licha ya kujua udanganyifu huo dhidi ya kampuni yake, amekaa kimya.
![]() |
Nembo bandia |
Tanzania PANORAMA Blog iliwasiliana na Kampuni ya Bright Choice Limited kupitia simu yake ya mezani ili kupata ufafanuzi wa madai hayo ambaye alieleza kuwa mwenye mamlaka ya kuzungumzia hilo ni mkurugenzi.
Afisa mmoja wa kampuni hiyo aliyejitambulisha kwa jina moja la Cecilia, kwanza alisema yeye ndiye msemaji kabla hajabadili na kusema ni afisa wa juu wa kampuni, alisema jambo hilo ni zito, mwenye mamlaka ya kulizungumzia ni mkurugenzi wake na pia alieleza kushangazwa na hatua ya waandishi wa habari kufuatilia jambo hilo wakati ni kazi ya Shirika la Viwango Tanzania (TBS)
Jitihada za kuipata menejimenti ya Kampuni ya Farmer’s Choice Limited ya Kenya kuzungumzia hilo zinaendelea.