![]() |
Msemaji Mkuu wa Serikali, Gerson Msigwa |
NA CHARLES MULLINDA
MWENENDO wa uchumi wa Taifa uko imara na hali ya ukusanyaji mapato kwa kipindi cha miezi mitano, kuanzia Januari hadi Mei, mwaka huu, haujatetereka.
Sambamba na hayo, mfumuko wa bei ni wa kiwango cha wastani wa asilimia 3.3 ambacho ni kiasi kizuri na akiba ya fuko la fedha za kigeni nayo imenona kwa kiwango cha kununua bidhaa na huduma kwa muda wa takribani miezi mitano.
![]() |
Dolla za Marekani |
Taarifa rasmi na za uhakika zilitolewa jana na Msemaji Mkuu wa Serikali, Gerson Msigwa kwa waandishi wa habari mkoani Dodoma zilieleza kuwa mwenedo wa uchumi wa Taifa ni mzuri licha ya kuwepo kwa mtikisiko mkubwa wa ugonjwa wa Corona.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, mwenendo wa ukuaji wa uchumi wa Tanzania sasa ni wa asilimia 4.7 tofauti na awali ulipokuwa ukikua kwa asilimia 6.9 kabla ya mtikisiko wa kiuchumi uliokumba dunia kutokana na ugonjwa wa Corona.
Ukuaji huo wa uchumi na kwa kuzingatia mwenendo wa uchumi za mataifa mengine duniani pamoja na athari za ugonjwa wa Corona, unaiweka Tanzania katika hali nzuri kwa wakati uliopo huku kukiwa pia na matarajio ya kuendelea kukua vizuri kwa uchumi kutokana na hatua madhubuti zinazochukuliwa sasa na Serikali ya Awamu ya Tano za kukabiliana na ugonjwa wa Corona.
Msigwa ambaye pia ni Mkurugenzi wa Idara ya Habari (Maelezo) alisema ukusanyaji wa kodi haujaterereka bali unakwenda vizuri na Serikali inawapongeza watanzania kwa kuitikia wito wa kulipa kodi bila shurti.
“Mwenendo wa makusanyo ya kodi kuanzia Januari 2021 hadi Machi 2021. Januari malengo yalikuwa Shilingi Trilioni 1.68 lakini kilichokusanywa ni Shilingi Trilioni 1.34. Kiwango hicho cha makusanyo ni sawa na asilimia 79.8.
“Mwezi Februari, 2021, malengo yalikuwa Shilingi Trilioni 1.61 lakini kilichokusanywa ni Shilingi Trilioni 1.33. Kiwango hicho cha makusanyo ni sawa na asilimia 82.9 na mwezi Machi malengo yalikuwa Shilingi Trilioni 1.99 lakini kiwango kilichokusanywa ni Shilingi Trilioni 1.67, sawa na asilimia 84.1,” alisema Msigwa.
Alitaja kiwango cha kodi kilichokusanywa na Serikali kwa mwezi Aprili kuwa ni Shilingi Trilioni 1.34 ikiwa ni chini kidogo ya malengo ya kukusanya Shilingi Trilioni 1.61 na kwa mwezi Mei, malengo ya makusanyo yalikuwa Shilingi Trilioni 1,619 na kiasi halisi kilichokusanywa ni Shilingi Trilioni 1.33, sawa na asilimia 82.