![]() |
Gerson Msigwa |
NA CHARLES MULLINDA
MSEMAJI Mkuu wa Serikali, Gerson Msigwa amemshukuru Rais Samia Suluhu Hassan kwa imani kubwa aliyoionyesha kwake kwa kumteua katika wadhfa alionao pamoja na kuwa Mkurugenzi wa Idara ya Habari (Maelezo).
Msigwa alitoa shukrani hizo jana katika mkutano wake na waandishi wa habari alipokuwa akitoa taarifa za mwenendo wa hali ya uchumi wa Taifa pamoja na utekelezaji wa majukumu ya Serikali katika kuuhudumia umma.
Sambamba na kumshukuru Rais Samia kwa kumuamini, pia aliwashukuru waandishi wa habari, wahariri na wadau wote wa habari kwa ushirikiano wanaompa tangu alipoteuliwa kushika wadhfa huo na jinsi wanavyoendelea kutekeleza jukumu lao la kutoa taarifa na aliahidi kuendelea kuwapa ushirikino.
Msigwa aliitumia pia fursa hiyo kueleza shukrani zake kwa Mwenyezi Mungu kwa kuivusha nchi salama katika kipindi kigumu cha msiba wa kitaifa na mabadiliko ya uongozi ambayo yalifanyika kwa amani na utulivu.
Alisema ni jambo la kumshukuru Mungu kwa nchi yetu kuheshimu Katiba na utawala wa sheria baada ya kifo cha Hayati Rais John Pombe Magufuli kutokea, aliyekuwa Makamu wa Rais, aliapishwa kuwa Rais kwa amani na utulivu mkubwa.
Akirejea rekodi zilizopo, alisema jana ilikuwa siku ya 80 tangu Hayati Rais Magufuli alipofariki dunia na siku ya 78 tangu Rais Samia Suluhu Hassan aingie madarakani.