![]() |
Mkuu wa Wilaya ya Arumeru, Jerry Murro akikagua nyaraka za wananchi (majina yao yamehifadhiwa kwa sababu maalumu) wenye migogoro ya ardhi katika wilaya yake |
MWANDISHI WA PANORAMA
WILAYA ya Arumeru imeanza awamu ya tatu ya utatuzi wa migogoro sugu ya ardhi yenye lengo la kuiunganisha kwa kuirejeshea amani jamii yenye migogoro na kujenga umoja.
Mkuu wa Wilaya ya Arumeru (DC) Jerry Muro, leo amewaambia waandishi wa habari kuwa awamu hiyo ya tatu ya utatuzi wa migogoro sugu ya ardhi itaongozwa na yeye mwenyewe, akishirikiana na wataalamu wa idara za ardhi pamoja na wanasheria wa Halmashauri za Arusha DC na Meru DC
DC Muro amesema awamu hiyo ni mwendelezo wa awamu zilizopita, ya kwanza na ya pili ambazo wakati wa utekelezaji wake ilibainika kuwepo haja ya kuendelea kutatua migogoro hiyo nje ya mahakama.
Amesema utafiti uliofanywa wakati wa utekeleza wa awamu ya kwanza na ya pili ya utatuzi wa migogoro ya ardhi, ulionyesha ipo migogoro mingi katika ngazi za kata na vijiji ambayo inahitaji kupatiwa ufumbuzi nje ya mabaraza ya kata na mahakama kwa sababu baadhi ya wananchi hawajui utaratibu wanaopaswa kufuata kupata haki zao za msingi zinazohusu migogoro ya ardhi.
![]() |
Mmoja wa wakazi wa Wilaya ya Arumeru (jina kapuni) akitoa maelezo kuhusu mgogoro wa ardhi anayodai kuwa ni mali yake lwa Mkuu wa Wilaya ya Arumeru, Jerry Murro (hayupo pichani) |
“Awamu ya tatu itakuwa ya kipekee kutokana na kuamua kwanza kutoa elimu kwa umma ya hatua wanazotakiwa kuchukua pindi kunapoibuka migogoro ya ardhi. Lakini pia tunakusudia katika awamu hii kuimarisha elimu kwa viongozi wa mabaraza ya ardhi ya kata ambao wanapaswa kuanza kusikiliza migogoro ya ardhi katika maeneo yao.
“Katika awamu ya kwanza na ya pili tulibaini wako baadhi ya wananchi ambao wametumia muda mwingi katika vyombo vya kisheria, hatua ambayo imeendelea kuongeza migogoro na usumbufu kwa wananchi.
“Pia tumebaini uwepo wa wananchi wasiokuwa na imani na mabaraza ya ardhi ya kata jambo ambalo linatoa nafasi kwa wachache kunufaika nayo na wapo baadhi ya wananchi ambao wanapenda sana kesi za migogoro ya ardhi,” alisema DC Murro.
Aidha, mkuu huyo wa wilaya amewaelekeza madiwani, watendaji wa kata na vijiji pamoja na wenyeviti wa vijiji na vitongoji kuungana nae katika awamu ya tatu kwa kusikiliza migogoro yote iliyobaki katika maeneo yao na kuipatia ufumbuzi katika kipindi cha miezi mitatu.
![]() |
Mkazi mwingine wa Wilayay ya Arumeru (jina kapuni) akitoa maelezo mbele ya Mkuu wa Wilaya, Jerry Murro ((hayupo pichani) kuhusu mggogoro wa ardhi aliyodai kuimiliki |