NA MWANDISHI WETU
KUNA utata wa nani mmiliki halali wa kiwanja namba 105, kilichopo eneo la viwanda huko Mbezi, Mkoa wa Dar es Salaam, ambacho mmoja wa wakurugenzi wa Kampuni ya Mohamed Enterprises Tanzania Limited (MeTL) Murtaza Alihussein Dewji alikiuza kwa Kampuni ya Ravji Construction Limited na pesa ya mauzo hayo ikachukuliwa na MeTL.
Msingi wa utata huo ni mzozo uliopo baina ya muuzaji Dewji, mnunuzi Kampuni ya Ravji Construction Limited, aliyechukua fedha za mauzo, Kampuni ya MeTL pamoja na Eugenia Rutatora na Wilson Mujwahuzi Rutatora waliokimbilia mahakamani kukidai kiwanja hicho baada ya kuuzwa, wakidai kuwa ni mali yao.
Dewji alikiuza kiwanja hicho kwa Kampuni ya Ravji Construction Limited na fedha za mauzo hayo zikachukuliwa na Kampuni anayoiongoza ya MeTL huku akishindwa kumpa hati ya kiwanja hicho mnunuzi na baadaye makachero wa polisi, kitengo cha uchunguzi wa makosa ya jinai kilitoa taarifa ya uchunguzi wa nyaraka za mauziano zilizowasilishwa na Dewji kuwa zilikuwa za kughushi
Kwa muda mrefu, Ravji Construction Limited, wamekuwa wakipasa sauti yao kuwa waliuziwa kiwanja hicho kwa njia za kitapeli wakiomba mamlaka za nchi kuwasadia kupata fedha zao walizoilipa Kampuni ya MeTL na pia wakitaka Murtaza afikishwe mahakamani kwa makosa ya kughushi nyaraka na saini za mauziano ya kiwanja hicho.
Taarifa zilizokusanywa na Tanzania PAMORAMA Blog kuhusu mgogoro huo zimeonyesha kuwa Murtaza aliuza kiwanja hicho huku akijua kuwa siyo mali yake na Kampuni ya MeTL ilipokea fedha za mauzo ya kiwanja hicho huku ikijua kuwa Mkurugenzi wake huyo si mmiliki halali wa kiwanja hicho.
Ingawa Murtaza anadaiwa kuwa na hati inayompa nguvu ya kisheria ya umiliki wa kiwanja hicho aliyopewa na mtu aliyeko nje ya nchi, Aliraza Kassamali Rajani, nyaraka nyingine zinaonyesha kuwa kiwanja hicho ni mali ya Eugenia Rutatora na Wilson Mujwahuzi
Nyaraka zilizoonwa na Tanzania PANOROMA Blog, zimeaonyesha kuwa Oktoba 22, 2010 Aliraza Kassamali Rajani wa sanduku la Posta 21545 Dar es Salaam alimpatia nguvu ya kisheria (Power of Attorney) Murtaza Alihussein Dewji ya umiliki wa eneo hilo.
Uchunguzi wa nyaraka hizo uliofanywa na Tanzania PANORAMA Blog umeonyesha zaidi kuwa kwa mara ya kwanza Rajani alisaini hati ya maombi ya nguvu ya kisheria mwaka 2010 na mwaka mmoja baadaye 2011 alisani hati ya kutoa nguvu ya kisheria kwa Dewji, lakini saini katika nyaraka hizo mbili zikiwa zimeacha maswali ambayo hajapata majibu kama ni za mtu mmoja yule yule au vinginevyo (Aliraza)
Mbali na kuwepo kwa utata huo, taarifa nyingine zimeonyesha kuwa muuzaji, Murtaza Dewji, hata baada ya Kampuni yake ya MeTL kupokea Dola za Marekani 600,000 za mauzo ya kiwanja hicho, hakukabidhi hati kwa muuzaji na badala yake alidai kuwa imepotea hivyo apewe muda wa kufanya mchakato wa kupata nyingine
Miaka miwili baadaye, kumbukumbu za maandishi zilizoonwa na Tanzania PANORAMA Blog zinasomeka kuwa mwaka 2013, Dewji aliandika barua kwenda kwa Msajili wa Ardhi, Wizara ya Ardhi akieleza kupotelewa na hati miliki ya kiwanja No 105 kilichokuwa na hati No 44512.
Dewji aliandika akiomba apatiwe hati mpya ya kiwanja namba 105 baada ya kupotelewa na hati yake ya awali.
Barua hiyo ilijibiwa Mei 13, 2013 ikiwa na kumbukumbu nambari LR/T/4451/17 na Afisa wa Wizara ya Ardhi, Bumi Mwaisaka akimtaka Dewji kutoa tangazo gazetini la kupotea hati hiyo kama sheria inavyoelekeza.
Imeelezwa kuwa wakati haya yote yakiendelea, familia ya Rutatola ambayo ni mmiliki wa kiwanja haikuwa na taarifa kuhusu kuuzwa kwa kiwanja hicho na baada ya kuvujishiwa taarifa hizo ilikimbilia mahakamani.
Familia ya Eugenia Rutatora na Wilson Mujwahuzi Rutatora ilikimbilia Mahakama ya Ardhi mwaka 2012 na kufungua kesi No. 141/2012 dhidi ya Manispaa ya Kinondoni, Ravji Construction Limited na Samson J. Mwaipaja
Familia hiyo ya Rutatora ilifungua shauri mahakamani la kuvamiwa kwa kiwanja chake namba 105 kilichopo Mbezi eneo la viwanda, chenye ukubwa wa ekari mbili na nusu.
Tanzania PANORAMA Blog itaendelea kukujuza zaidi kuhusu sakata hili.