![]() |
Rais Dk. John Magufuli |
NA MWANDISHI WETU
KAMPUNI ya Ravji Construction ya mkoani Kilimanjaro imemuomba Rais Dk. John Magufuli kuingilia uchunguzi wa malalamiko ya kugushi nyaraka iliyoyatoa polisi zaidi ya miaka mitano sasa ili haki iweze kutendeka.
Akizungumza na Tanzania PANORAMA Blog hivi karibuni, mmoja wa maofisa wa kampuni hiyo aliyeomba jina lake lihifadhiwe kwa kile alichodai kuwa ni kuhofia usalama wake, alisema kampuni yake inaamini haki haiwezi kutendeka mpaka Rais Dk. Magufuli atakapoingilia kesi hiyo.
Alisema imani hiyo inatokana na uwezo mkubwa wa kifedha alionao mlalamikiwa aliyemtaja kuwa ni Kampuni ya METL na kwamba ripoti ya uchunguzi huo inayoonyesha jinsi mmoja wa maafisa waandamizi wa METL alivyogushi nyaraka na sahihi za kampuni ya RAVJI, imefichwa tangu mwaka 2014.
“Inabidi sasa nijitokeze kulalamika ili Rais Magufuli asikie sauti yetu atutetee, atusaidie. Ni miaka mingi sana sasa tumedhulumiwa na huyu tajiri wa METL, na hapa zipo kesi mbili, moja ya kutudhulumu ardhi ambayo tulinunua kutoka kwake lakini pili ni kughushi nyaraka.
“Sisi tulilalamika polisi kuwa afisa wa juu wa METL anayefahamika kwa jina la Murtaza Dewji aligushi nyaraka na sahihi za bosi wetu, polisi walifanyia uchunguzi madai yetu, aliyepepeleza shauri hilo ni ASP Chrisantus Kitandala, aliyekuwa kitengo cha Forensic Bureau, alichunguza hatua zote zilizoghushiwa na Murtaza.
“Baada ya uchunguzi huo, bosi wake, Kamishna wa Forensic Bureau, Nestory Tagaya aliandika ripoti kwa mkuu wa upelelezi wa Kawe akieleza bayana kuwa Murtaza aligushi nyaraka na sahihi za kampuni yetu, hiyo ilikuwa 2014 lakini baada ya ripoti hiyo mpaka leo hali ni kimya tu, hakuna hatua zilizochukuliwa dhidi ya waliobainika kugushi.
“Baba yangu ni mgonjwa sana, alipoteza mabilioni ya pesa kwa sababu ya vitendo hivyo vya kugushi vilivyofanywa na afisa wa METL, anaweza kufa wakati wowote, yupo Arusha sasa, naomba mnisaidie kupaza sauti rais asikie ili asaidie hatua zichukuliwe haki yetu ipatikane kwa sababu watu hawa waliotenda haya ni wakubwa,” alisema.
Jitihada za kumtafuta Murtaza kuzungumzia tuhuma hizo hazikufanikiwa baada ya Tanzania PANORAMA Blog kufika ofisini kwake mara mbili na kuelezwa kuwa hayupo.
![]() |
Gulam Dewji |
Mmiliki wa Kampuni za METL, Gulam Dewji alipotafutwa ofisini kwake naye ilielezwa kuwa hayupo na hawezi kupatikana kwa muda usiofahamika na hata alipotafutwa kwa simu yake ya kiganjani kuzungumzia suala hilo alisema anaumwa, yupo nyumbani, hivyo hawezi kuzungumza chochote.