NA MWANDISHI MAALUM – ARUMERU
Mkuu wa Wilaya ya Arumeru (DC) Jerry Muro amemtaka mkandarasi anayetekeleza mradi wa maji katika Halmashauri ya Arusha kuukamilisha ndani ya siku 30 ili kutotoka nje ya mkataba.
Akizungumza katika eneo linapojengwa tanki kubwa la kuhifadhi maji alikofanya ziara ya kukagua maendeleo ya ujenzi wake, DC Murro alisema ameridhishwa na maendeleo yake lakini mkandarasi anapaswa kuhakikisha anaumaliza ndani ya siku 30 zilizosalia kama inavyoelekezwa kwenye mkataba.
Amesema amefanya ziara hiyo baada ya kutokea changamoto ya kupasuka kwa mabomba kila maji yanapofunguliwa kutoka kwenye tanki kubwa lililopo juu, changamoto ambayo imepatiwa ufumbuzi katika ziara hiyo.
“Mradi huu una thamani ya zaidi ya shulingi bilioni tisa na tangu umeanza kutekelezwa sasa tumebakiza siku 30 kwa ajili ya mradi huu kukamilika lakini nimeona unaenda vizuri ndiyo maana nikasema tutembee ili tuone wapi kuna changamoto ili tuweze kuzitatua kabla ya siku 30 hizi hazijafika tukabidhi mradi.
“Mpaka sasa nataka niwahakikishie zaidi ya asilimia 50 ya maji yameishaingia kwenye mzunguko lakini changamoto kubwa hapa ilikuwa kupasuka kwa mabomba. Ukifungua maji kutoka juu yakishuka mabomba yanapasuka, sasa nikaona hapana lazima nije mwenyewe nijue kwanini yanapasuka. Leo, tumalize ule mzizi wa fitina tujue kwa nini mabomba yanapasuka.
“Sasa tuna habari njema, moja kati ya sababu zilizokuwa zinasababisha mabomba kupasuka ni presha ya maji kutoka juu pale mlimani kwenye tanki kubwa kwa sababu maji yanashuika kwa kasi kwa sababu yakishuka kwa kasi yakikuta wewe hujafungua maji yanajaa yanapasua mabomba, lakini changamoto hii leo tumeimaliza na hamtaiona tena katika maisha yenu. Sasa tunaendelea kuongeza mlazo wa mabomba,”alisoma DC Murro.
Mradi huu mkubwa utahudumia vijiji vitano vilivyo katika Kata ya Ngaramtoni, Lemanyata na Oludonywasi vyenye wakazi zaidi ya 50,000 watanufaika na unatekelezwa kwa ushirikiano wa Serikali ya Tanzania na Serikali ya Uingereza kupitia Shirika la Water Aid.
Katika ziara hiyo, DC Murro aliambatana na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Arusha, Mbunge wa Arumeru magharibi, Mwenyekiti wa Halmashauri ya Arusha, wawakilishi la Shirika la Water Aid na watendaji wengine wa serikali na mamlaka za maji.