Saturday, April 19, 2025
spot_img

MBATIA POPO WA KISIASA ALIYECHUJA

 
Mbatia
HUWEZI kuandika ukurasa mmoja wa historia ya harakati za vijana katika kutafuta na kujenga mageuzi ya Taifa hili bila kuandika jina James Francis Mbatia. Huu ndiyo ukweli ingawa kwa baadhi yetu hatupendi kuusuikia.

Nimeanza kwa kuukiri ukweli huu kwa sababu wahenga wana msemo wao usemao “mnyonge mnyongeni lakini haki yake mpeni.” Hivyo pamoja na ukweli kwamba sasa anaonekana kupwaya katika nafasi nyeti aliyonayo ya kiongozi wa chama cha upinzani.

Mbatia ni miongoni mwa Watanzania waliojitolea sehemu kubwa ya muda na nafasi zao kushiriki harakati za ujenzi wa mageuzi ya kisiasa katika taifa letu.

Ninamfahamu Mbatia tangu mwanzo wa harakati zake miaka ya 1991 katika kambi ya upinzani. Nilimfahamu na niliendelea kumfahamu hata alipofanikiwa kuingia bungeni na baadaye alipoukosa mwaka 2000. Lakini katika kipindi chote hicho sikupata kufikiri kuwa atakuja gharimu muda wangu kumjadili hasa kwa mambo ya hovyo.

Sikupata kufikiri hivyo kwa sababu mwanzoni mwa harakati zake alijipambanua kamakijana mweledi na mpigania haki wa kweli miongoni mwa vijana. Alikuwa na misimamo isiyoyumba na alifanikiwa kujenga imani kubwa miongoni mwa vijana wenzake na hata kwa watu wazima.

Lakini ni bahati mbaya sana baada ya kushindwa ubunge mwaka 2000 na chama kuanza kupita kwenye wakati mgumu wa kufanya siasa katika mazingira ya ukata, ndipo nilipoanza kuushuhudia upopo wa kisiasa wa Mbatia.
Ni kipindi hicho, ndipo alipoanza kuwa mwanasiasa mwenye kutumia akili sana katika kushabikia na kushadadia watalawa na wenye fedha. Staili aliyoitumia katika kutekeleza hilo ni kujifanya mtaifa aliyepitiliza na mwanasiasa asiyefungamana na siasa kali.

Kwa wenye akili, wanajua kuwa ukiona mwanasiasa wa upinzani aliyekuwa na msimamo thabiti wa mwelekeo wa kimapinduzi anaanza kucheza na maneno ya utaifa huku akipunguza hasira za raia waliochoka na kukata tamaa, mwanasiasa huyo anakuwa mfu.

Na kwa Mbatia tangu kushindwa kwake ubunge mwaka 2000 alianza kujidhirisha kwa wanamageuzi wa kweli kuwa zama zake za kuwa miongoni mwa majemedari vijana katika kambi ya upinzani zilikuwa zimekwisha. Katika upinzani alikuwa mwanasiasa mfu.

Ili kuondoa dhana inayoweza kujengeka miongoni mwa mashabiki wake kuwa ninamuweka katika kundi la wanasiasa mfu wa kambi ya upinzani kwa sababu binafsi ninataja sababu za kuamini kuwa kwa sasa ni mwanasiasa mfu.

Mosi, baada ya chama cha upinzani chenye nguvu visiwani Zanzibar, CUF, kukataa kumtambua Rais Amani Karume, mwaka 2000, Mbatia aliibuka na kauli tata aliyowashangaza wanamageuzi na wasiokuwa wanamageuzi kwa sababu wengi waliokuwa wakifuatilia uchaguzi ule walikiri kwamba rais Karume hakushinda kihalali.

Akiwa mmoja wa viongozi wa chama cha upinzani ambao kazi yao kubwa ni kuwaongoza wafuasi wao kukiondoa chama tawala madarakani, aliibuka na hoja kwamba kutomtambua rais aliyetangazwa na Tume ya uchaguzi ni uhaini kikatiba.

Inawezekana ni kweli lakini nani asiyejua kwamba utawala wa CCM ulitengeneza katiba kwa maslahi ya chama hicho? Kwa wenye kufikiri sawasawa, hoja hii ya Mbatia ilikuwa na maslahi gani kwa NCCR Mageuzi zaidi ya kujenga mazingira ya kuonekana kuwa ni chama kinachotumiwa?

Kwangu mimi, hilo lilikuwa doa jeusi la kwanza kwa Mbatia. Nilianza kupata shaka na mwenendo wake kisiasa.

Lakini Mbatia hakuishia hapo, hata baada ya machafuko ya kisiasa na uchaguzi kurudiwa mwaka 2003, Mbatia alifanya kituko kingine ambacho kwa wafuatiliaji wa siasa wa kambi ya upinzani watakubaliana na mimi ingawa hakuna ushahidi wa wazi, lakini shaka kuwa alifanya hivyo kwa maelezo maalumu, haiwezi kupuuzwa.

Mbatia, huku akijua kuwa anacheza mchezo mchafu kisiasa aliwawekea pingamizi wagombea wa CUF kule Zanzibar. Kwa mtu mwenye akili timamu hapo unaweza kujiuliza Mbatia alikuwa anataka nini kwa wanaCUF? Pingamizi lile aliliweka kwa sababu ya ujinga, kutekeleza matakwa ya waliomtuma au alikuwa na kisasi na watu wa CUF?

Maswali haya yanajengwa katika ukweli kwamba Mbatia kama mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi alikuwa anajua fika kuwa chama chake hakikuwepo Zanzibar hivyo hakikuwa na wagombea. Hakikuwa na cha kupoteza badala yake kama ilivyo ada kilipaswa kuwaunga mkono CUF. Ajabu kikawapinga. Kwa maana nyingine kilitaka chama tawala kiendelee kutawala.

Historia iko wazi katika hili, kuwa tangu kuanza kwa mfumo wa vyama vingi hapa nchini Zanzibar ina vyama viwili tu vinavyoshindana kuchukua dola, Chama Cha Mapinduzi (CCM) na CUF.
Vyama vingine vya CHADEMA, NCCR-Mageuzi, TLP, JAHAZI, nk, viko Zanzibarkutokana na masharti ya muungano tu.

Zanzibar hakuna chama nje ya CCM na CUF kilicho ongoza hata kitongoji. Matokeo ya uamuzi ya Mbatia kuwawekea pingamizia wagombea wa CUF ni moja ya sababu zilizowasukuma wanachama wa chama hicho kupiga kura za maruhani kwa sababu hawakuitaka CCM wala NCCR Mageuzi.

Na katika uchaguzi huo, Mbatia na chama chake hawakuvuna kitu kutokana na uamuzi wao wa ukibaraka? Lakini anayepaswa kulaumiwa katika hiloni Mbatia.

Leo hii, ninapowasikia vijana wapambanaji katika kambi ya upinzani kupitia CUF wakimtaja Mbatia kuwa Mwenyekiti wa CCM ingawa hawafafanui ninaamini kuwa wanampa cheo hicho kwa sababu wanamuona si mwenzao katika kambi ya upinzani, bali ni pandikizi wa CCM katika upinzani.

Mbatia mwenyewe, naamini kwa sababu ya kuisha na pengine kwa sababu anafahamu kuwa kinachosemwa ni kweli hajajitokeza kukanusha kauli hiyo. Tunachopaswa kujiuliza wachokonozi kutokana na kauli hiyo ya wanaCUF ni kwamba Mbatia ni Mwenyekiti wa CCM Mkoa gani? au Wilaya gani? au Tawi gani? au ni kweli kwamba NCCR Mageuzi ni tawi la CCM?

Kwa sababu hiyo, nikitambua kuwa NCCR-Mageuzi ni chama cha upinzani, sikushangaa niliposikia kauli ya wazee wa chama hicho ya kumtaka Mbatia apumzike. Kwangu niliona huo ni mwanzo wa ufufuko wa chama hicho.
Niliamini hivyo kwa sababu ninakubaliana nao kuwa Mbatia anapaswa kuondoka sasa katika wadhfa wa uenyekiti kwa hiari yake au kwa kulazimishwa, ninaamini hivi kutokana na imani nyingine niliyo nayo kuwa kiwango ambacho watawala wamemtumia Mbatia kimempausha kisiasa, kimemfanya asitamanike tena miongoni mwa wanamageuzi.

Kwa wanamageuzi wa kweli, kulitaja jina la Mbatia kuwa mmoja wa majemedari wa kambi ya upinzani ni kituko.
Ni kituko kwa sababu wakati majedari wa kweli wa upinzani wakiongozwa na Dk. Wilbroad  Slaa kutangaza orodha ya majina ya waliowaita mafisadi, Septemba 2007, Mbatia aliibuka na hoja eti Watanzania wote ni mafisadi isipokuwa wanatofautiana viwango.
Ingawa huo ulikuwa mtizamo wake lakini kwa kiongozi wa ngazi aliyonayo. Kauli hiyo kwa Watanzania waokufa kutokana na viongozi kuendekeza ufisadi ni sawasawa na tusi!
Hapa mtu anaruhusiwa kujiuliza maswali kadhaa ili kumuelewa Mbatia, kuwa lengo la kauli yake hiyo dhidi ya viongozi wenzake wa upinzani lilikuwa nini?
Sidhani kama ni dhambi kukubaliana na wazee wa NCCR-Mageuzi wanaotaka kumfuku kwenye ulaji alionao kwnia lengo la kauli hiyo ilikuwa kupunguza hasira za wananchi dhidi ya viongozi wa CCM waliotajwa kwenye orodha ya mafisadi.

Kauli za namna hii ndiyo zimewafikisha Watanzania kwenye kupoteza imani dhidi ya Mbatia na chama chake. Ni mwenendo wa namna hii uliosababisha apoteze imani kwa wanamageuzi wenzake nchini.

Huo ndiyo msingi wa kushindwa kwake kila anapogombea tangu awe mwenyekiti anashindwa. Watu wake wana imani na upinzani lakini hawana imani na yeye kwa sababu ya upopo wake kisiasa.

Nyingine Zinazohusiana na Hii

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Tufuatilie

0FansLike
3,913FollowersFollow
0SubscribersSubscribe
- Advertisement -spot_img

Habari Nyingine Mpya