Na Simba Gembagu Ng’wana Njamiti
Ninakita ili nijikite lakini sijikiti badala yake ninakitwa. Ninatafuta pa kukita ili nipate pa kujikita na kuutangazia ulimwengu kuwa ingawa nimekuwa nikiweweseka kwa muda mrefu kutokana na kukosa mahali pa kukita, sasa nimepapata. Nimejikita.
Lakini matokeo ya takwimu ya sensa yalinimaliza nguvu. Nikiwa nimejikita kuyaperuzi, nilijikuta ninakitwa na ongezeko kubwa la mimba za utotoni na ukubwani.
Na nilipojikita kuchunguza chanzo cha watanzania kujazana mimba kama hawana akili nzuri nilibaini kuwa ni mikito ya ukakasi wa maisha inayozidi kukita kila kukicha.
Hebu twende pamoja ili kila ninapokita tukite pamoja. Tuzikite akili zetu kufikiri pamoja kwa kawaida tu kuwa ni kwanini watanzania wanapeana mimba kwa fujo kiasi cha takwimu za hesabu yao kuonyesha kuwa wameongezeka kwa kasi wakati kasi ya ukuaji wa uchumi wao na ustawi wao kisiasa ukididimia.
Tuzifikirishe akili zetu kuwa ni kwanini watanzania wanazaliana sana licha ya kutokuwa na uhakika wa maisha yao ya kesho! Majibu ya haraka ingawa ni mepesi yanayopatikana ni haya.
Watanzania hawataki kufanya kazi kwa sababu wamekulia katika mazingira ya kutofanya kazi. Siyo wote lakini wengi wamekulia katika mazingira ya aina hiyo. Kwao hawa maisha yanakwenda kiujanja ujanja.
Watanzania hawa wavivu wa kufanya kazi wana bidii ya kupeana mimba. Mazingira wanakopigia porojo yanahamasisha upeanaji mimba kwa sababu mara nyingi wanakuwa baa au sehemu nyingine za starehe. Inaeleweka, starehe ni pamoja na kugawiana mimba.
Hata kama ni mchana kukiwa na mwangaza mkali wa jua shurti milango na madirisha ifungwe ili kuwe na giza. Kama ni mwanga basi utaruhusiwa kuwepo kidogo sana.
Kuna mamia ya watanzania wanaopenda kufanya kazi lakini wanashindwa kwa sababu ya kukosa mwanga unaozalishwa kwa nishati ya umeme ambayo serikali imeshindwa kuhakikisha upatikanaji wake wa uhakika.
Mfano wa uongo huo ni ule wa profesa anayesimamia upatikanaji wa umeme ambaye alitangaza hivi karibuni kuwa kwa sababu yeye ni profesa na amechaguliwa kusimamia umeme ambao kwa miaka nenda rudi umekuwa adimu kupatikana, atauprofesa umeme ili upatikane kwa uhakika. Hautakosekana tena.
Hivyo kwa sababu ya giza, watu wakiwa majumbani hawawezi kuangalia televisheni au kusikiliza redio na badala yake hujifungia vyumbani mapema na kulala gizani. Matokeo yake ndiyo hayo, mimba.
Na kwa sababu watu wengi wanapenda simulizi za kupeana mimba, nani kafumaniwa na nani na nani kachumbiwa na nani, kaolewa au yuko na nani. Matokeo ya maongezi haya huwasukuma watanzania ambao sehemu kubwa ya maisha yao ni giza kujikita katika kugawiana mimba.