Imekuwa kita nikukite, umekuwa mwendo wa mikito. Wakubwa kwa wadogo wanakitana kwa staili tofauti tofauti. Hayupo asiyejua kukitwa au kukita. Watanzania wamekuwa watu wa kukitana usiku na mchana.
Aliyekitwa safari hii ni mzee wa Mikito, amekitwa mkito dhaifu kwa nyuma kisha wakitaji wake wakatoka mbio kwa hofu ya kukitwa kwa mbele huku wakishangilia ukitaji wao dhaifu waliomkita mzee wa Mikito.
Kwa sauti za kukoroma zilizokuwa zikitoka kwenye midomo iliyoumbwa katikati ya sura zilizopauka, waliomkita walikoroma kwa kulalama kuwa amekiuka miiko ya chamani ya kufichiana siri.
Kwa umoja wao chamani wakaungana kumkita mzee wa Mikito, wakajikita katika kumsomea mashtaka ya uongo na kweli yaliyojikita kwenye uzushi, upotoshaji na uzandiki wa kusikitisha. Kisha wakamuhukumu hukumu ya kusimama.
Kama ilivyo desturi ya wana mikito, mzee wa kukitwa hakukubali kukitwa, akajikita kwenye utetezi alioujenga kwa hoja za nguvu zilizowatikisa wakitaji wake wakatikisika, wakajawa hofu kwa mitikisiko ya hoja zile.
Kujinusuru wasikitwe, wakaisimamia hukumu yao ya kusimama. Wakageuka wakukitwa.
Wahenga walisema, anayekubali kushindwa ni mshindani. Mzee Mikito kwa sababu ni mshindani akakubali kushindwa, akajisimamisha milele chamani kwa sababu hakuwa mmoja wao bali mtalii. Alikwenda chamani kutalii na kufaidi vinono vya kitalii. Basi!
Wana viherehere mashabiki wa wana mikito, wanapenda sana kushabikia kukitana. Hata kabla mzee Mikito hajajikita kuwakita wakitaji wake kwa hoja zenye mashiko, wenyewe wamejikita kukusanya taarifa zote za siri za wakitwaji, ili wampelekee kwa ahadi ya kuzitumia kuwakita wa kukitwa.
Ukiwatizama walivyojikita kufanya kazi hiyo, utawaona wakiwa hawana tofauti na wanawake vizabizabina wa mwembe tongwa ambao kila wanalolinusa, wanalifikisha kwa mjumbe.
Wanazoa siri za chamani zinazoonyesha kuwa kile kinachoitwa chama siyo chama, bali ni utapeli wa Mtaa wa Kongo wa kuuziwa kipande cha simu kilichotengenezwa kwa kipande cha sabuni.
Hakuna kabati la wa kukitwa linaloachwa wazi, yote yanafunguliwa na kupigwa sachi kusaka vielelezo vilivyofichwa na matarishi wa wenye viliba tumbo ambayo yanaonyesha jinsi walivyo wanafiki na walivyoumbwa kwa roho za plastiki ambazo zikikutana na moto mkali kidogo zinayeyuka.