Sunday, June 22, 2025
spot_img

RAIS KIKWETE, DADA JOYCE MCHOKOZI


RAFIKI yangu Rais Jakaya Kikwete, ninaleta mashtaka kwako. Ninamshtaki Dada Joyce Mapunjo, ananichokoza. Ananitisha kwa kutumia kaukubwa ulikompa katika ofisi yetu.
Mashtaka haya nayaleta kwako kwa nia njema kabisa, nataka umkataze hiyo tabia ya uchokozi kwa sababu akiendelea nayo, ataniudhi. Nikiudhika na mimi nitamchokoza. Ikiwa hivyo, tutakuwa tunachokozana na matokeo ya kuchokozana hayatakuwa mazuri.
Rafiki yangu Rais Kikwete, uchokozi wa Dada Joyce ni huu; ametuma vijana wake aliona pale ofisini ulipomuweka waje wanifanyie fujo kwa kutumia mwamvuli wa ukubwa uliompa. Wamekuja kunichokoza katika ofisi yangu ya huku uswahilini kwa wachokonozi.
Ni jambo la bahati nzuri kwamba vijana wa Joyce hawakunikuta. Wangenikuta, nadhani nisingewaacha hivi hivi, walah naapa! Lazima ningewatupa katika selo niliyonayo hapa ofisini wakati nikiendesha uchunguzi wa kisa cha kuja kunichokoza.
Ingawa nimeelezwa kuwa walikuja kigaidi hivyo uwezekano wa kuwa magaidi ni mkubwa, hilo lisingenipa taabu kwa sababu dawa ya gaidi ni kumdhibiti mapema kabla hajajitoa mhanga kwa kujilipua au kukulipua.
Dada Joyce aliwatuma vijana wake kuja kukagua nyaraka za kibiashara za ofisi ndogo ninayoisimamia sasa baada ya kuapa kwa miungu yake yote kwa mwajiri wangu kuwa atatumia mbinu za kigaidi kuniangamiza. Kisa! Kiherehere changu cha kusema ukweli kuwa ana tamaa, ni mdhulumaji na anatumia ukumbwa uliompa vibaya.
Natambua kuwa Dada Joyce hakupenda madudu anayoyafanya hapo wizarani alipo sasa yafahamike lakini hili la kuwa na tamaa iliyopitiliza hata kufikia hatua ya kuwa mdhulumaji nilishindwa kulifumbia macho.
Najua hata wewe rais ukisikia jinsi anavyoichafua ofisi uliyompa kuiongoza utakasirika kwa sababu anachokifanya si kuichafua ofisi hiyo na yeye binafsi, bali serikali nzima unayoiongoza wewe rafiki yangu. Hata hivyo nakuomba usifike huko kwenye kukasirika ili nikusimulie jinsi Watanzania wako wanavyonyanyaswa na huyu dada.
Iko hivi; mfanyabiashara mmoja mdogo, anaitwa Jaffer Ole Koimere pamoja na washirika wenzake wanne, Februari 26, 2010 walianzisha kampuni ya kutoa nembo ya utambuzi wa bidhaa ‘Bar Codes’ na kuipa jina la GS1 Tanzania Limited kabla ya kupewa hati ya usajili namba 75537, hapo Machi 18, mwaka huo huo na Wakala wa Usajili wa Biashara Tanzania (BRELA).
Sasa cha kuchekesha baada ya Dada Joyce kugundua jitihada za walalahoi hao, alimwalika Koimere ofisini kwake kwa mazungumzo. Katika mazungumzo hayo, Dada Joyce alikiri mbele ya Koimere kuifahamu Kampuni GS1 Tanzania Limited na azma yake. Na hakuacha kumsifia Koimere na wenzake kwa jitihada zao za kubuni na kuanzisha Kampuni ya Barcodes.
Baada ya kuwasifia, bila aibu! akamuomba Koimere amuachie kampuni hiyo kwa sababu anaitamani sana kutokana na faida itakayokuwa inamuingizia halafu eti !yeye atamsaidia mambo mengine. Koimere alikataa.
Binafsi jambo hilo lilinishtua mno, kusikia Dada Joyce licha ya ukubwa uliompa unaomuwezesha kuishi maisha bora bado anatamani vya wenzake wanaopigana juani kuyakimbia maisha magumu. Nilimdharau kweli kwa jinsi alivyojidhalilisha kwa kuonyesha alivyo mtu wa tamaa na kibaya zaidi, jinsi alivyoshushuliwa na Koimere kwa kumkatalia ombi lake.
Dada Joyce aliposhushuliwa alikasirika, akapanga kufanya dhuluma. Kwanza aliandika barua Brussels, Ubelgiji yaliko Makao Makuu ya GS1 Global kueleza kuwa kampuni ya mjasiriamali Koimere haitambuliwi serikalini kisha akaitambulisha kampuni ya GS1 (TZ) National Limited iliyosajiliwa ghafla Machi 28.
Halafu pamoja na upuuzi mwingine uliofanyika hapo katikati kuhusu kusajiliwa kwa kampuni mpya ambayo Dada Joyce alionyesha kila dalili za kuibeba mno jambo linaloashiria kuwa na yeye ana mkono humo kutokana na tamaa aliyoionyesha. Akashiriki kutumia mamilioni ya fedha za serikali kufanikisha usajili wake huku akijua kuwa kampuni hiyo ni binafsi.
Hili ndilo jambo lililoniudhi kiasi kwamba kiherehere changu kilipanda hadi kufikia hatua ya kuwaambia vijana wangu tupayuke ovyo kuutangazia umma jinsi Dada Joyce anavyotumia madaraka yake vibaya.
Zipo taarifa kuwa Kaka Chami, yule uliyemuweka kuwa juu ya Dada Joyce alisikia madudu aliyokuwa akiyafanya, akakasirika na kuandika barua kali akionya kuachwa mara moja kwa mchezo huo mchafu.
Nilipata bahati ya kuiona barua ya Kaka Chami, haikuwa na mambo ya kulemba, ilikuwa ikieleza wazi kuwa amegundua kampuni inayokingiwa kifua na Dada Joyce ni ya binafsi na uanzishwaji wake umetumia rasilimali za serikali zikiwemo fedha.
Barua ya Kaka Chami pia ilielekeza mamilioni ya fedha za Serikali ambazo ni kodi ya Watanzania zilizotumika katika vikao vya kuanzisha Kampuni ya GS1 (TZ) National Limited zirejeshwe kwa sababu ni kampuni binafsi.
Halafu anaonyesha shaka kuwa kama ufumbuzi hautapatikana na haki ikatendeka, dhuluma hiyo itaichafua BRELA, Wizara na Serikali ya CCM kwani kuna kila dalili kuwa Kampuni ya GS1 Tanzania Ltd ikienguliwa kwa staili hiyo ya udhulumaji, itaishia kuishtaki BRELA/Wizara.
Wasiwasi huu wa Kaka Chami ulinifanya nijipe jukumu la kuhahakisha Koimere na wenzake hawaendi mahakamani ili kuinusuru serikali yetu kuzidi kuchafuliwa kwa sababu ya tamaa ya Dada Joyce. Na kwa sababu hiyo, nikaona ni jambo la busara kuuambia umma kuwa katika hili tatizo sio serikali bali Joyce.
Rafiki yangu Rais Kikwete, naamini unatambua vema jinsi serikali yetu inavyoandamwa sasa na wapinzani na hata wenzetu tulionao kundini. Hawa tulionao kundini wametuchukia kwa sababu ambazo kila mtu anazijua na sasa wameungana na wapinzani wetu kutuchafua.
Wanafanya kila lililo ndani ya uwezo wao na wanatumia kila njia, nzuri na mbaya kuhahakisha tunachukiwa na wananchi. Kisa nao wanautaka ukubwa ili wafaidi.
Maskini, hawajui kuwa badala ya kufaidi ukubwa ulionao, unataabika kwa sababu mzigo wa maisha magumu ya Watanzania wako umekulemea.
Sasa ukiwa katika hali hiyo ya mateso na kutaabika, anapojitokeza Dada Joyce na kutaka kukuongezea mateso kwa kuwafanya watu wako waendelee kuichukui serikali. Kisa anatamani vya kwao! Nadhani jambo hili halikubaliki.
Tena, kwa kiburi kwa kijivuni, huku akijua kuwa anakukosea wewe uliyempa kimvuli cha kula kiulani. Anatumia ukubwa uliompa kututisha wachokonozi kwa sababu hatukubaliani na vitendo vyake vya tamaa na dhuluma ambavyo gharama yake ni anguko la serikali yetu.
Itoshe tu hapa kufikisha mashtaka haya kwako nikikuomba kuwa, ingawa najua utakasirika sana kwa kusikia ukweli huu lakini usimfukuze kazi kwa sababu lawama zote ataziangushia kwangu.
Kwa sababu wewe ndiye uliyemteua unayo mamlaka ya kumkanya kuhusu mwenendo wake huu na hasa tabia yake ya tamaa na dhuluma. Pia asipende kunichokoza kwa sababu madhara yatakayompa nikiiga tabia yake ya uchokozi, tukaanza kuchokozana ni makubwa.
Na kama hatakusikia, nakuomba niachie. Nitamchokoza kwa kumchokono mwenendo wake binafsi na wa kikazi na kwa kiherehere changu cha kawaida nitawatangazia Watanzania wote nitakayoyagundua kwenye uchunguzi wangu huo.

Nyingine Zinazohusiana na Hii

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Tufuatilie

0FansLike
3,913FollowersFollow
0SubscribersSubscribe
- Advertisement -spot_img

Habari Nyingine Mpya